WAPIGA kura katika jimbo la Liwale mkoani Lindi pamoja na kata nne za Tanzania Bara wametakiwa kujitokeza kwa wingi kupiga kura katika uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika kesho Jumamosi tarehe 13 Oktoba 2018. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 12 Oktoba 2018 na Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Semostocles Kaijage ambapo amewatoa hofu wapiga kura huo, kwamba uchaguzi utakuwa wa amani na utulivu.
Jaji Kaijage amewataka viongozi wa vyama vya siasa, wagombea na wafuasi wao na wananchi kwa ujumla kujiepusha na vitendo vinavyoweza kusababisha fujo na au vurugu katika vituo vya kupigia, kuhesabia na kujumlishia kura.
“Wananchi waheshimu Sheria za Nchi wakati wote wa upigaji, kuhesabu, kujumlisha kura na kutangaza matokeo. Pale panapokuwa na malalamiko yoyote ya ukiukwaji wa Sheria na Taratibu za Uchaguzi, malalamiko hayo yafikishwe kwenye mamlaka inayohusika kwa utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa Sheria.”, amesema Jaji Kaijage na kuongeza kuwa:
“Ni wajibu wa vyama vya siasa vinavyoshiriki katika uchaguzi kuweka mawakala katika vituo vyote vya Kupigia na Kujumlishia Kura kwa utaratibu ambao tulikubaliana na umekuwa ukitumika katika chaguzi za hivi karibuni wakati wa Mkutano wa Tume na Vyama vya Siasa tarehe 10/07/2018 uliofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam, na maelekezo kuhusiana na utaratibu huo kutumwa kwa Wasimamizi wa Uchaguzi.”, amekumbusha Jaji Kaijage.
Aidha, Jaji Kaijage amesema upigaji kura utafanyika kuanzia saa moja kamili asubuhi na kumalizika saa kumi kamili jioni katika vituo vilivyotumika wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na kwamba watakaokuwepo kwenye mstari kwenye vituo vya kupigia kura kuanzia saa kumi kamili jioni wataruhusiwa kupiga kura.
Leave a comment