TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) leo tarehe 4 Agosti, 2018 imetangaza Uchaguzi Mdogo wa Ubunge katika majimbo matatu na wa udiwani katika kata mbili za Tanzania Bara utakaofanyika Septemba 16, mwaka huu. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Akitangaza uchaguzi huo mjini Dodoma leo, Makamu Mwenyekiti wa NEC, Jaji Mbarouk Salim Mbarouk amesema fomu za uteuzi wa wagombea wa Majimbo hayo zitatolewa kuanzia tarehe 13 hadi 20 Agosti, 2018 na uteuzi utafanyika tarehe 20 Agosti, mwaka huu wakati kampeni zitaanza tarehe 21 Agosti na kumalizika tarehe 15 Septemba, mwaka huu.
“Tume ilipokea barua kutoka kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambaye kwa kuzingatia kifungu cha 37(3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, aliitaarifu Tume uwepo wa nafasi wazi za Ubunge katika Majimbo matatu,” amesema Jaji Mbarouk.
Jaji Mbarouk ameyataja majimbo hayo kuwa ni Korogwe Vijijini, Mkoa wa Tanga kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo Ndugu Stephen Hilary Ngonyani, Jimbo la Ukonga Katika Mkoa wa Dar Es Salaam na Jimbo la Monduli katika Mkoa wa Arusha
Amesema wabunge wa majimbo hayo mawili Ndugu Mwita Mwikabe Waitara na Ndugu Julius Kalanga Laizer wajiuzulu uanachama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na hivyo kupoteza sifa za kuwa Wabunge.
Leave a comment