CHAMA cha NCCR-Mageuzi nchini Tanzania kimeoneshwa kusikitishwa na kauli ya Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) Simon Sirro aliyesema ataweka kambi visiwani Zanzibar, kwa ajili ya kufuatilia Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Hivi karibuni akiwa katika ziara ya kikazi visiwani huo, IGP Sirro aliahidi kuweka kambi Zanzibar kwa ajili ya kudhibiti baadhi ya watu watakaofanya fujo katika uchaguzi huo, ili kuhakikisha amani na usalama inakuwepo.
Haji Ambar Khamis, Mgombea mwenza wa urais wa Tanzania kupitia NCCR-Mageuzi akizungumza kwenye uzinduzi wa kampeni za urais viwanja vya Zakhiem-Mbagala jijini Dar es salaam, amemuomba IGP Sirro amuombe Mungu alinde amani ya Taifa badala ya kutoa kuali za kuwatia hofu wananchi.
“Tunamuomba IGP Sirro huko aliko, asiwatishe wananchi, arudi akaombe dua kanisa tubaki salama, Mungu ndiye muombwa, kauli zake si vyema, wananchi wa Pemba watajiona wanyonge,” amesema Khamis.
Wakati huo huo, Khamis amemuomba Rais wa Zanzibar, Ali Mohamed Shein kuhakikisha uchaguzi huo unakuwa huru na haki ili aiache Zanzibar salama.
“Mimi ni Mzanzibar, Rais Shein wakati anaingia madarakani mwaka 2010 mimi nilikiwa katika watu wa mwazo waliompongeza Shein, mimi nilikuwemo, hakuna uchaguzi uliofanyika mzuri hata sisimizi hakufa kama uchaguzi wa 2010.”
“Sisi tunasema anayekufadhili ndio wenzako, Rais Shein alifadhiliwa na Wazanzibar akachagulia katika uchaguzi huru, akaingia madarakani salama, atuache salama,” amesema Khamis.
Pia, Khamis amemuomba Rais John Magufuli aimarishe demokrasia hususan katika kipindi hiki cha uchaguzi.
“Rais John Magufuli anapongezwa sana na dunia nzima kwa kutumbua majipu, kwamba ni mtumbuaji mkubwa wa jipu lakini jipu lililoiva ndilo linalotumbuliwa huwezi kutumbua bichi. Jipu lililoiva ni demokrasia ambalo ameshindwa kutumbua,”amesema Khamis.
Naye mgombea urais wa NCCR-Mageuzi, Yeremia Maganja amemuomba IGP Sirro kuwa makini na kauli zake zinazochochea wengine.
“Simon Sirro, usiwashe kiberiti katika majani makavu. Simon Sirro anajua. Sisi Tanzania tutahakikisha imavuka salama, tunailinda amani yetu,” amesema Maganja
Leave a comment