BARAZA la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) limevitaka vyuo na taasisi za elimu kutoa matokeo ya wahitimu wao mapema kwa ajili ya kuwarahisishia kupata Namba ya Uhakiki wa Tuzo (AVN) itakayowawezesha kujiunga na elimu ya juu kwa wakati husika. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 24 Agosti, 2018 na Twaha A. Twaha, Mkuu wa Kitengo cha Udahili NACTE wakati akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
Twaha amesema kuwa, baadhi ya wahitimu wamekuwa wakikwama kupata AVN kwa wakati husika kutokana na vyuo na au taasisi zao kutowasilisha mapema matokeo yao halisi NACTE.
“Kumekuwepo na malalamiko ya baadhi ya wahitimu wa ngazi ya stashahada na hasa waliomaliza masomo yao kwa mwaka wa masomo 2017/2018 hadi mwezi Julai, 2018.
Baadhi ya wahitimu hao mara tu baada ya kumaliza mitihani yao na kupatiwa matokeo ya awali wamekuwa wakiomba AVN kwa kuambatanisha hati za matokeo ya awali wakati vyuo na taasisi husika hazijawasilisha NAVTE matokeo halisi yaliyoidhinishwa na mamlaka husika,” amesema Twaha na kuongeza.
“Na pia uhakiki wa matokeo yao haujakamilika kwenye mfumo wa uhakiki wa Tuzo wa Baraza. Ifahamike kwamba hakuna mhitimu wa ngazi ya diploma anayeweza kujiunga na elimu ya juu bila kuwa na AVN.
“Huu ni utaratibu uliowekwa na baraza ili kurahisisha utambuzi wa tuzo za elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchini.”
Leave a comment