MCHUNGAJI wa Kanisa la Maombezi (GRC), Antoni Lusekelo maarufu kama ‘Mzee wa Upako’, amekivaa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kuhusu misimamo yake juu ya mlipuko wa Virusi vya Corona. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mei Mosi mwaka huu, Chadema kupitia mwenyekiti wake, Freeman Mbowe, kiliwaagiza wabunge wake kutohudhuria vikao vya bunge vinavyoendelea jijini Dodoma, kwa madai ya kutoridhishwa na namna serikali inavyolishughulia janga hilo.
Akitangaza marufuku hiyo, Mbowe aliwataka wabunge hao kujiweka karantini kwa muda wa siku 14, ili kuangalia kama hawajaambukizwa ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na virusi hivyo (Covid-19).
Pia, aliushauri uongozi wa bunge, kusitisha shughuli zake, kisha kuwapima wabunge na watumishi wa mhimili huo, ili kujua mwenendo wa Covid-19, sambasamba na kudhibiti ueneaji wake.
Msimamo huo wa Chadema ulifuata baada ya wabunge watatu, Mbunge Viti Maalumu, Mchungaji Getrude Lwakatare, Balozi Augustine Mahiga, aliyekuwa Waziri wa Katiba na Sheria, na Richard Ndassa, Mbunge wa Sumve, kufariki dunia.
Hata hivyo, uongozi wa bunge ulisema wabunge hao hawakufariki dunia kutokana na ugonjwa wa Covid-19.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari leo tarehe 12 Mei 2020, Mzee wa Upako amedai kuwa, wabunge walioamua kutoka bungeni ni wasaliti katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Corona.
“Hawa “People’s Power” mwaka huu katika uchaguzi wataona nguvu ya Umma itakavyo wageukia, kwa kuwa ni wasaliti hawatopata kura ya mbunge wala diwani. Wataenda kulima kahawa makwao” amesema Mzee wa Upako.
Wakati huo huo, Mzee wa Upako amemtaka Rais Mstaafu wa Zanzibar, Aman Abed Karume, kumuonya binti yake, Mwanasheria Fatma Karume, aache kutumia vibaya jina la Karume, katika upotoshaji juu ya taarifa ya janga la corona.
“Amani Karume muonye binti yako tena binti wa kiislamu, ametoka familia stahiki yenye heshima kwenye nchi yetu, asitumie hata jina la Karume kuchafua hata jina la familia” ameseza Mzee wa Upako.
Mchungaji huyo amewataka watanzania kushikama na kuwa wamoja kulikabili janga hili na kuacha Siasa kwani Corona itapita lakini Tanzania itabaki pale pale.
Leave a comment