TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Manyara, inamshikilia Patrick Joakimu Kauky kwa kosa la kufanya ubadhirifu wa vifaa vya ujenzi wa Ikulu ndogo, unaoendelea wilayani Hanang’. Anaripoti Mwandishi Wetu, Manyara … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatatu tarehe 22 Juni 2020 na Holl Makungu, Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Manyara.
Makungu amesema TAKUKURU inamsaka Mhandisi Dominicianus Kilina, Mhandisi wa mkoa wa Manyara, ambaye anadaiwa kula njama na mzabuni huyo.
Makungu ameeleza kuwa, mzabuni huyo aliyepewa tenda ya kutengeneza madirisha ya aluminium na Ofisi ya Manunuzi mkoani Manyara, alifanya udanganyifu kwa kutengeneza madirisha yaliyo chini ya kiwango, ikilinganishwa na fedha alizopewa.
Makungu amesema mtuhumiwa huyo anadaiwa kutengeneza na kuweka madirisha yenye kioo chenye unene wa 5mm badala ya 6mm kama mkataba wa makubaliano yao unavyoelekeza.
Makungu amesema kabla ya mzabuni huyo kukamatwa, TAKUKURU ilimuagiza asiendelee kuweka madirisha hayo hadi pale yatakapofanyiwa ukaguzi ili kubaini kama amebadili viwango na ubora wake, lakini alikaidi.
Makungu amesema baada ya TAKUKURU kuweka zuio hilo, mzabuni huyo alimweleza Mhandisi Kilina, , ambaye alielekeza madirisha hayo yawekwe haraka na kabla ya hayajakaguliwa.
“TAKUKURU mkoa wa Manyara tulipata taarifa ya kudharau maelekezo yetu, na nikaelekeza mzabuni na mafundi wake waliokutwa wametekeleza agizo la mhandisi huyo wakamatwe kwa uchunguzi,” amesema Makungu na kuongoza:
“wakati Mhandisi Kilina akitafutwa kusaidia uchunguzi huo, Kilina bado hajapatikana kwa kuwa tulielezwa kuwa yuko nye ya Babati kikazi.”
Leave a comment