ALI Hassan Mwinyi, Rais mstaafu wa awamu ya pili, ameshauri matumizi ya Katiba ya Tanzania yasitishwe kwa muda ili kumpa nafasi Rais John Magufuli, kuendelea kuongoza nchi katika kipindi cha mpito. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Rais Mwinyi ametoa ushauri huo leo Jumamosi tarehe 11 Julai 2020, katika Mkutano Mkuu wa CCM, unaofanyika jijini Dodoma.
Rais Magufuli amechaguliwa tena na Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), kugombea Urais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020, ambapo anatafuta nafasi ya kumalizia muhula wake wa pili ili kukidhi matakwa ya Katiba ya Tanzania.
Hata hivyo, leo wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM wanapiga kura ya kumthibitisha Rais Magufuli kuwa mgombea wa urais wa chama hicho, katika uchaguzi huo.
Mwenyekiti huyo wa CCM alianza safari yake ya uongozi wa muhula wa kwanza tarehe 5 Novemba 2015, baada ya kushinda katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2015.
Akizungumza kwa niaba ya Marais wastaafu, Mwinyi amesema, licha ya kwamba Katiba ya Tanzania inapaswa kuenziwa, lakini kutokana na mambo mazuri aliyoyafanya Rais Magufuli, anatakiwa kuongezewa muhula mmoja, kama asante ya uongozi wake kwa Taifa.
“Nchi yetu ina katiba na katiba lazima tuienzi, tusiingilie lakini tukitaka tunaweza kuighairisha kwa muda mfupi ili kumpa rais wetu huyo kipindi kingine kimoja cha asante ,” amesema Rais Mwinyi.
Mwinyi amesema, Rais Magufuli amekuwa kiongozi wa mfano kutokana na kufanikiwa kutekeleza miradi mikubwa ambayo wengine walishindwa kufanya.
“Sote tumeshuhudia toka umeingia rais wetu kafanya mengi makubwa mengine ya ajabu. Sijasikia nchi isiyokuwa na hela kuweza kununua ndege 11 kwa pesa za ndani, sijasikia nchi masikini ikathubutu kushughulikia haya aliyoyashughulukia mengine nimeyasahau, “ amesema Mwinyi
“Mcheza kwao hutunzwa, ningetaka mambo mawili, kwa hakika kufikiriwa na hakika tuhakikishe tunashawishi Watanzania wenzetu rais wetu huyu apate matokeo mazuri,” amesema
Baada ya kumaliza, Rais Magufuli huku akifurahia alisema, Rais Mwinyi kwa nini marais wastaafu hawakuongeza muda, akiwemo yeye, Benjamini Mkapa na Jakaya Kikwete.
“Asante sana Mzee Mwinyi, mbona wewe hukukubali kuongeza siku zilizokuwa zimebaki? Au Mzee Mkapa mbona hakuongeza? Lakini nimekuelewa wewe ni mtani wangu asante sana,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment