ALI Hassan Mwinyi, Rais mstaafu wa awamu ya pili wa Tanzania, amemwomba Mwenyezi Mungu kumsamehe Hayati Benjamin William Mkapa pale alipoteleza wakati wa uhai wake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Lupaso…(endelea).
Akizungumza baada ya kupewa nafasi hiyo na Rais John Magufuli wakati wa kutoa salamu za mwisho kijijini Lupaso, Mtwara, Mwinyi amesema, Mzee Mkapa naye ni mtu hivyo kuna mahali hukutenda aliteleza.
“Ndugu yetu marehemu Mkapa ni mwanadamu kama walivyo wengine, labda katika maisha yake aliwahi kufanya kosa asilolipenda muumba wetu.
“Katika hali kama hii, mwenzetu akiondoka, jambo la kwanza ni kumuombea usalama kwa Mwenyezi Mungu endapo kakosea. Kaanza kukosa baba yetu Bwana Adam, basi kama ana kosa, Mwenyezi Mungu amsamehe,” amesema.
Mwinyi ametoa pole kwa Mama Anna, Mjane wa Mkapa ndugu na jamaa kutokana na msiba huo, akisema miongoni mwa mambo anayokumbuka kutoka kwa Mzee Mkapa nikutokuwa na mchezo kazini.
Hata hivyo, Mzee Mwinyi amesema, kwenye shughuli hiyo kuna jambo amelikumbuka katika miaka ya nyuma, hata kama wengine wanaweza kuliona dogo.
“Mnaweza kuona ni jambo dogo, lakini kuna jambo ambalo nimeliona hapa. Nyinyi nyote mmevaa viatu, kwangu hili jambo si dogo.”
“Mimi nilivyaa viatu mara mbili, mara ya kwanza nilipokwenda jandoni nikiwa na miaka 13 na mara ya pili nilipovuna karafuu nikapata hela nikanunua viatu,” kauli hii ilimfanya Rais Magufuli na wengine kuangua kicheko.
Leave a comment