MWILI wa Rais mstaafu wa awamu ya tatu wa Tanzania, Benjamin William Mkapa leo Jumatatu tarehe 27 Julai 2020 unalala nyumbani kwake, Masaki jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mwili huo umetolewa uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam saa 12 jioni kwenda nyumbani kwake, Masaki na tayari umekwisha kufika.
Kesho Jumanne asubuhi, mwili huo utaondolewa nyumbani hapo na kupelekwa Kanisa Katoliki la Imaculata, Upanga kwa mida na baadaye utapelekwa Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam kwa ajili ya shughuli ya kuagwa kitaifa.
Shughuli hiyo ya Kitaifa ya kumuaga Mkapa (81), itahudhuriwa na wananchi pamoja na viongozi mbalimbali wa ndani na nje nchi, wakiongozwa na Rais wa Tanzania, John Magufuli.
Mkapa aliyezaliwa tarehe 12 Novemba 1938, alifikwa na mauti Alhamisi tarehe 23 Julai 2020 katika moja ya hospitali jijini Dar es Salaam kwa mshituko wa moyo na atazikwa kijijini kwake Lupaso, Masasi Mkoa wa Mtwara.
Mkapa alikuwa Rais wa Tanzania kwa miaka kumi mfululizo kuanzia mwaka 1995 hadi 2005.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online, MwanaHALISI TV na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali
Leave a comment