TAASISI ya Sekta Binafsi nchini (TPSF) imeendelea kuwahimiza wadau waliyopo kwenye sekta hiyo kufuata sheria, taratibu na uzalendo ili kuepukana na vitendo vya rushwa ndani ya sekta hiyo kwa manufaa ya Taifa. Anaripoti Moses Mseti, Mwanza … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo na Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Salum Shamte wakati wa mkutano wa majadiliano baina ya sekta binafsi kwa mikoa ya kanda ya ziwa ilioyofanyika jijini Mwanza.
Shamte alisema kuwa serikali imekuwa na malalamiko ya muda mrefu kuhusu maadili ndani ya sekta binafsi, hivyo ni wakati sasa wa wadau hao kuanza kukabiliana na tatizo hilo mapema kwa ukuaji wa maendeleo ya nchi.
Alisema upungufu ndani ya sekta binafsi ndiyo sababu serikali inaamua kufanya udhibiti uliopiliza ambao alidai unasababishia hasara kwenye sekta binafsi kutokana na ukosefu wa maadili ndani yao.
“TPSF na sekta binafsi nzima tuna jukumu la kuhamasisha uadilifu ndani ya sekta binafsi ili kuwe na kanuni za maadili (Code of Conduct) ambazo zinalenga kupunguza udhibiti uliopitiliza unaofanywa na serikali na kuelekea kwenye dhana ya udhibiti binafsi kama ilivyo kwenye nchi nyingi zinazoendelea vizuri kiuchumi.
“Jambo hili kwa hakika limechangia sana kwa pande mbili hizi kutokuaminiana hivyo tujadiliane swala hili na hatua gani zichukuliwe ili kurudisha imani kwa serikali yetu na sisi wenye tuweze kunufaika,” alisema Shamte.
Pia Shamte aliwataka wadau na washiriki wa mkutano huo kujadili mambo yenye tija ikiwamo mapendekezo ya namna ambavyo sekta binafsi itashiriki katika utekelezaji wa muongozo wa marekebisho ya kanuni za udhibiti ili kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara maarufu kama Brueprint.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa TPSF, Godfrey Simbeye alimpongeza Rais John Magufuli kwa kufanya majadiliano yenye tija kati ya sekta ya umma na sekta binafsi ambayo amedai yameleta mafanikio makubwa ikiwemo katika sekta ndogo ya zabibu kupunguziwa tozo kwenye mchuzi wa zabibu zinazolimwa nchini.
Simbeye aliyataja mafanikio mengine kuwa ni pamoja na kuanza kwa utekelezaji wa mpango kazi wa kuboresha upatikanaji wa leseni na mazingira ya biashara kwa ujumla yaani Brueprint kupitia sheria ya fedha ya mwaka 2019/20 ilioanza kutumika Julai mosi mwaka huu.
Leave a comment