REHEMA Mikidani Ngenje, Mwanafunzi wa Darasa la Nne Shule ya Msingi Somanga, Lindi amemweleza Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli, shule yao ilivyo mbovu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Somanga, Lindi … (endelea).
Rehema amefikisha kilio hicho mbele ya Rais Magufuli leo Alhamisi tarehe 30 Julai 2020, wakati kiongozi huyo wa nchi aliposimama eneo hilo kusalimia wananchi akiwa anakwenda Dar es Salaam.
Rais Magufuli anatokea Lupaso, Masasi mkoani Mtwara alikokuwa akiongoza mazishi ya Hayati Benjamin William Mkapa jana Jumatano.
Mkapa alifariki dunia Alhamisi iliyopita tarehe 23 Julai 2020, saa 3:30 usiku kwa mshtuko wa moyo.
Akiwa eneo la Somanga, Rais Magufuli ameuliza kama kuna matatizo yoyote, ndipo alipouliza kama kuna mwanafunzi eneo hilo. Rehema akajitokeza na kisha akapewa kipaza sauti.
Bila kutoa salamu, Rehema ameanza kumwagika “shule yetu mbovu sana, madawati hakuna. Sementi imebomoka bomoka, kwanza shule yenyewe mbovu.
“Mabati yote yameshakuwa na kutu, shule yooote sasa hivi mbovumbovu, rangi zote wanazopaka sasa hivi zimeishafutika.”
Rais Magufuli: Inaitwa shule gani mwanangu?
Rehema: Shule ya Msingi Somanga.
Kisha Rais Magufuli ameuliza kama kuna mwalimu wa shule hiyo, hata hivyo aliendelea kumuuliza binti huyo.
Rais Magufuli: Sogea hapa mwanangu, upo darasa la ngapi?
Rehema: Darasa la Nne
Rais Magufuli: Basi naichangia hiyo Shule ya Msingi Somanga Sh. 5 milioni.
Rais Magufuli: Sogea hapa mwanangu. Unaitwa nani?
Rehema: Rehema Mikidadi Ngenje
Rais Magufuli: Ninatoa miloni 5, lakini Sh.100,000 ubaki nayo wewe. Naitoa hapa, mpandishe huyu mtoto (anamkabidhi),
Rais Magufuli: Siku moja na wewe uwe waziri au uwe rais, sawa mwanangu?
Pia, Rais Magufuli amepokea zawadi ya kuku kutoka kwa mkazi wa eno hilo, aliyemsubiri ili kumpa zawadi hiyo.
“Nimeletewa kuku wangu na mzee, nampokea mimi mwenyewe halafu nampelekea mama yangu. Tena mzuri kweli, asante sana.”
“Mzee ngoja na mimi nikupe zawadi, embu nisaidie Sh.100,000. Haya na mimi nakupa Sh.100,000 ikusaidie, Mungu akubariki kwa upendo, akusaidie Somanga sintoisahau,” amesema.
Leave a comment