ALIYEKUWA Mwanafunzi wa kidato cha tano katika shule ya Sekondari Sengerema mkoani Mwanza, Ayoub Yahya (19) amekutwa amefariki dunia baada ya kujinyonga asubuhi ya leo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Tukio hilo limethibitishwa leo tarehe 18 Oktoba 2018 na Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, ACP Advera Bulimba.
ACP Bulimba ameeleza kuwa, mwanafunzi huyo alijinyonga kwa kutumia kamba ya chandarua aliyokuwa ameifunga kwenye mti uliopo pembeni ya uwanja wa mpira wa shule ya Sekondari Sengerema.
Ameeleza kuwa, wanafunzi wenzie ndiyo waliotoa taarifa baada ya kupita uwanjani hapo na kumuona akiwa amefariki kisha wakatoa taarifa kwenye uongozi wa shule ambao ulifikisha taarifa za tukio hilo katika kituo cha polisi.
“Chanzo cha mauaji hayo bado hakijafahamika, Polisi bado tunaendelea na uchunguzi kuhusiana na tukio hilo. Mwili wa marehemu umehifadhiwa hospitali ya DDH Sengerema kwa ajili ya uchunguzi, pindi uchunguzi ukikamilika utakabidhiwa kwa ndugu wa marehemu kwa ajili ya mazishi,” amesema ACP Bulimba.
Leave a comment