HARRISON Mwakyembe, aliyekuwa mbunge wa Kyela kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), ametahadharisha kwamba kujaa watu kwenye mikutano si hoja ya kushinda. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kyela…(endelea).
Akizungumza na wanachama wa chama hicho kwenye uzinduzi wa kampeni za jimbo hilo, jijini Mbeya amewataka wanachana hao kwenda kupiga kura tarehe 28 Oktoba 2020.
Amewataka wanachama hao kuacha kulumbana na badala yake, wasake kura za urais, mbunge na madiwani wa jimbo hilo.
Katika kura za maoni ndani ya CCM, Dk. Mwakyembe aliangushwa na Ally Mlaghila ambaye ndiye aliyepitishwa na chama hicho kugombea ubunge katika jimbo hilo.
“Ushindi haupatikani kwa wingi wa watu kujaa mikutano ya kampeni, bali kwa wingi wa kura,” amesema Dk. Mwakyembe.
Amesisitiza kuachana na dhana kwamba, ushindi tayari umepatikana kutokana na kutekelezwa kwa miradi mingi kwenye utawala wa Rais John Magufuli.
Hata hivyo, amewaomba wana Kyela kumpa kura Dk. Magufuli ambaye ni mgombea urais wa CCM, kutokana na juhudi zake za kuibadili Kyela na kuwa na taswira ya maendeleo.
Leave a comment