MVUA inayoendelea kunyesha mfululizo jijini Dar es Salaam, imesababisha mawasiliano ya barabara kukatika kwenye baadhi ya maeneo ya jiji hilo. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Alfajiri ya leo tarehe 13 Mei 2019, Barabara ya Kawawa ilifungwa kutokana na Bonde la Mkwajuni kujaa maji. Barabara nyingine iliyofungwa kwa sababu hiyo ni ile ya Morogoro katika eneo la Jangwani.
Magari yanayopitia katika barabara Kawawa, yalilazimika kubadili njia, ikiwemo magari yanayoelekea Makumbusho, Masaki, Mawasiliano na maeneo mengine ya jiji.
Daladala za Mbagala, Gongolamboto, Temeke, Buza, Tandika, Kariakoo, Mbagala, Mabibo, Tabata yalishindwa kupita mkwajuni na badala yake yaliazimika kufika Mwananyamala A na kuingia Tandale kwa Mtogole kisha kwenda Magomeni ili kuindelea na safari.
Daladala za kwenda Kawe, Morocco nazo zililazimika kupitia njia ya Tandale kwenda Mwananyamala A kisha kuendelea na safari.
Hali Kadhalika, Barabara ya Morogoro maeneo ya Jangwani ilifungwa kutokana na kujaa maji, kufuatia hatua hiyo, safari za kuelekea Kivukoni, Gerezani na Muhimbili kupitia eneo hilo zilisimamishwa.
Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (Udart) imesitisha huduma zake za usafiri kwa muda kutokana na maeneo hayo kujaa maji.
Udart kupitia kwa Mkuu wa Idara ya Mawasiliano, Deus Bugaywa alitoa taarifa ya kusitishwa kwa huduma hizo, akisema kwamba kampuni hiyo itatoa huduma kwa safari za Kimara-Mbezi na Kimara-Magomeni Mapiga, Gerezani-Muhimbili na Kivukoni Muhimbili.
Pia mabasi ya kwenda Kilimanjaro, Dodoma, Iringa, Mbeya, Songea, Kigoma, Mpanda, Kagera, Morogoro na maeneo mengine yamebadilisha njia na kwamba, yanatoka Ubungo kwenda Mwenge, kisha Tankibovu na kuchukua Barabara ya Goba kwenda hadi Mbezi na kisha kuendelea na safari.
Maeneo mengi ya jiji la Dar es Salaam maji yametuama kutokana na hata mafuriko kutokana na mvua iliyonyesha mfululizo kuanzia usiku was aa 5 mpaka alfajiri ya leo
Leave a comment