MTOTO Miriam Michael (6) mkazi wa Ilembo kata Nsalala wilaya ya Mbeya amefariki dunia baada ya kula mboga za majani zinazodhaniwa kuwa na sumu, anaandika Esther Macha.
Kamanda wa Polisi wa Mkoani Mbeya, Dhahiri Kidavashari amesema kuwa tukio limetokea Juni 13, mwaka huu majira ya saa 18.00 jioni huko Ilembo.
Kidavashari amesema kwamba mtoto huyo alikuwa anasoma chekechea alifariki muda mfupi baada ya kufikishwa katika hospitali Teule ya Ifisi kwa matibabu.
Akizungumzia zaidi tukio hilo Kidavashari amesema marehemu alifikishwa hospitalini hapo akiwa na mtoto mwenzake aitwaye Felister Mussa (7) wote walifikishwa hospitali kwa ajili ya matibabu.
“Katika tukio hili walikuwa watoto wawili lakini mtoto aliyefariki ni mmoja na huyu mwingine bado yupo hospitali ya Ifisi anaendelea na matibabu,” amesema Kamanda Kidavashari.
Aidha Kidavashari amesema kuwa inadaiwa kuwa chanzo cha kifo hicho ni baada ya marehemu na mwenzake kula mboga za majani aina ya maboga ambazo inadaiwa zilipikwa kwenye chombo ambacho kinasadikiwa kilitunzia sumu ya kuulia wadudu ambayo bado haijajulikana.
Hata hivyo kamanda huyo amesema kuwa hali ya kupoteza fahamu ilitokea wakati marehemu na mtoto mwenzake wakicheza baada ya kula na kuanza kulegea na mwili kukosa nguvu.
“Mtoto Felister Mussa bado amelazwa hospitali Teule Ifisi akiendelea na matibabu na hali yake inaendelea vizuri mwili wa marehemu umefanyiwa uchunguzi wa kitabibu na kukabidhiwa ndugu kwa mazishi,” amesema Kamanda.
Leave a comment