TISHO la virusi vya corona limebadili utaratibu wa maisha duniani. Mfano ulio wazi ni Jiji la New York, Marekani wikiendi iliyopita. Inaripoti mitandao ya kinataifa … (endelea).
Eneo ambalo watu walikuwa wakienda kustarehe kwa michezo mbalimbali, sasa limezungushiwa viduara na kwa anayetaka kuwepo eneo hilo, anapaswa kukaa ndani ya duara lake.
Hakuna uhuru wa kutembeatembea, kula wala kunywa eneo hilo, wanaofika pale kwa sasa wanaruhusiwa ‘kupiga stori’ tu ndani ya kiduara chao walichokikuta na kisha kuondoka.
Maisha katika viwanja vya ‘Domino Park’, yamebadilika, sasa hakuna kurukaruka na michezo ya hapa na pale, hakuna kupigana vikumbo, utii wa umbali wa mita sita umezingatiwa.
Viwanja vya Domino Park ni maarufu sana jijini humo kwa watu kukutana na kupumzika, majani yaliyopandwa na kutunzwa vizuri, mwanga wa kutosha na utulivu wake uliwafanya wakazi wa jiji hilo kuzuru mara kwa mara.
Kila wikiendi, eneo hilo lilikuwa limejaa watu wa aina mbalimbali, ni eneo linalovutia wapenzi kwenda kupumzika na hata ahadi ya makutano kutokana na umaarufu wake.
Viduara vilivyozungushwa kwenye viwanja hivyo, vina futi sita vikitosha watu wawili mpaka wanne. Lengo ni kuendelea na kupambana na maambukizi mapya ya virusi vya corona kwakuwa umbali unaokubalika.
Jiji hilo ambalo limeripoti zaidi ya visa 200,000, licha ya masharti ya kukaa ndani kulegezwa, wakazi wa New York wameshauriwa kuendelea kukaa ndani iwapo hawana ulazima wa kutoka.
Mtindo wa kuweka alama kutoka mtu na mtu umeimarishwa maeneo malimbali ikiwa ni pamoja na madukani, ofisini, hotelini, migahawani na sehemu za biashara.
Mpaka sasa, Marekani ndio taifa la kwanza linaloogoza kwa wagonjwa zaidi ya 1.4 milioni wa corona na vifo vilivyotokana na ugonjwa huo.
Leave a comment