DAKIKA 90 zimemalizika dimba la Jamhuri mkoani Morogoro kwa mabingwa watetezi wa ligi kuu Vodacom Tanzania Bara 2020/21, Simba kutoshana nguvu kwa kufungana 1-1 na Mtibwa Sugar. Amaripoti Mwandishi Wtu, Morogoro … (endelea)
Ulikuwa mchezo wa kushambuliana kwa zamamu na hadi timu hizo zinakwenda mapumziko, Simba ilikuwa ikiongoza 1-0 goli lililofungwa dakika ya 45 na kiungo wa mabingwa hao, Mzamiru Yassin kwa shuti kali.
Mtibwa walisawazisha goli hilo dakika ya kwanza ya kipindi cha pili yaani dakika ya 46 kwa kichwa cha Boban Zirintusa akiunganisha mpira kona.
Simba imefikisha pointi nne katika michezo miwili iliyocheza ya ligi baada ya mchezo wa awali wa ufunguzi wa ligi kushinda 2-1 dhidi ya Ihefu FC katika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.
Kwa Mtibwa Sugar, hii ni sare yake ya pili ikiwa nyumbani baada ya ile ya ufunguzi dhidi ya Ruvu Shooting iliyomalizika kwa kutofungana.
Nahodha wa Simba, John Bocco amesema “Tunamshukuru Mungu tumemaliza salama mchezo, tumepata pointi moja, tunaangalia makosa tuliyoyafanya ili mechi ijayo yasijirudie lakini Mtibwa wamecheza vizuri kipindi cha pili.”
Kuhusu ushindani wa ligi ya msimu huu baada ya kuchezana michezo miwili, Bocco amesema “ushindani utakuwepo.”
Naye Issah Rashid, Nahodha wa Mtibwa Sugar amewaomba mashabiki wa timu hiyo kuendelea kuwaunga mkono kwa kwenda uwanjani ili kuwawezesha kufanya vizuri.
Katika mchezo mwingine uliochezwa Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam kati ya KMC na Tanzania Prisons imemalizika kwa KMC kupata ushindi wa 2-1.
Huu ni ushindi wa pili mfululizo kwa KMC baada ya ule wa awali wa 4-0 dhidi ya Mbeya City kwenye uwanja huo huo.
Tanzania Prisons kikiwa ni kipigo cha kwanza baada ya mchezo wa awali dhidi ya Yanga kutoka 1-1 katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Leave a comment