JULIUS Mtatiro, Mkuu wa Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, amewaonya watendaji watakaokwamisha minada ya korosho. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Mtatiro ametoa onyo hilo baada ya kubaini changamoto mbalimbali zinazokwamisha minada hiyo, ikiwemo ukosefu wa vifungashio vya korosho, pamoja na wanunuzi kupata usumbufu katika kushiriki minada hiyo.
Mkuu huyo wa Wilaya ya Tunduru, amewataka viongozi wa Vyama vya Msingi (TAMCU) wilayani humo, kuhakikisha changamoto hizo zinatatuliwa, kabla ya siku ya mnada, ambayo ni Alhamisi ya tarehe 28 Novemba, 2019 na wasipotekeleza agizo hilo, ataweka rumande.
“Mwenyekiti na meneja wa TAMCU, maghala mengi niliyotembelea mengi hayana magunia, yamekwama Dar es Salaam, kesho meneja wa TAMCU na mwenzio, nikiwakuta mko Tunduru nawaweka ndani,” amesema Mtatiro na kuongeza;
“Kwa hiyo kama gari lako halina mafuta, panda mabasi uende Dar es Salaam, nataka magunia yaingie ya kutosha.”
Wakati huo huo, Mtatiro amelitaka Jeshi la Polisi Wilayani Tunduru, kuhakikisha wafanyabiashara wanaoingia wilayani humo kwa ajili ya kushiriki kwenye minada ya korosho, hawawekewi vikwazo.
“Wanunuzi wa korosho nimepata maoni yenu, malalamiko yenu kwamba mnavyosafiri kutoka Mtwara kuingia Tunduru ili kubidi katika mnada, mnapata matatizo barabarani.
Naagiza polisi kuhakikisha kila siku ya Alhamisi ambapo wanaingia Tunduru kuwaletea wakulima fedha, wasisumbuliwe na askari yeyote wa barabarani waingie moja kwa moja Tunduru,” ameagiza Mtatiro.
Mtatiro amesema katika mnada wa wiki hii, wakulima wa Tunduru wameuza kilo 2.976 milioni ambazo zenye thamani ya zaidi ya Sh. 8.2 bilioni.
Leave a comment