WADAU wa Jukwaa la Katiba Tanzania wamesema kuwa taifa haliwezi kuwa na maendeleo kama halitakiwa na dira ya maendeleo inayoeleweka,” anaandika Dany Tibason.
Kauli hiyo imetolewa leo na Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Ruaha Prof. Gaudens Mpangala wakati wa mafunzo ya wanachama wa Jukwaa hilo kuhusu hatma ya mchakato wa Katiba Mpya Tanzania.
Licha ya kuwa Tanzania haina dira kwa sasa pia Mhadhiri huyo amesema bila kurudisha mchakato wa Katiba Mpya ya Tanzania, yenye maoni ya wananchi hakuna maendeleo ambayo yanaweza kupatikana.
Prof. Mpangala amesema kuwa kwa sasa hali ya demokrasia imeminywa na kwamba wananchi hawana maamuzi yoyote.
Amesema demokrasia iliyopo kwa sasa ni kupiga kura, lakini baada ya kumalizika kwa uchaguzi Watanzania wengi wamekuwa hawana demokrasia hatua inayosababisha washindwe kujieleza au kukosoa mambo mbalimbali ambayo yanatakiwa kuhojiwa.
“Lazima kujua kuwa kuna nguzo tatu za demokrasia ambazo ni Mamlaka ya wananchi, Ushiriki wa wananchi pamoja na Ukombozi kwa wananchi”amesema
Prof .Mpangala amesema kwa sasa haki za binadamu hazifuatwi kwa kuwa yapo mambo ambayo yanaendelea kujitokeza ikiwa ni pamoja na Mahakama na Bunge kuingiliwa badala ya vyombo hivyo kusimamia haki ambazo zinatakiwa.
Amesema inafahamika wazi kuwa Bunge linatakiwa kuisimamia serikali lakini kwa bahati mbaya kwa sasa serikali imekuwa ikilisimamia jambo ambalo si la Kidemokrasia.
“Tunajua wazi kuwa kwa sasa serikali ya awamu ya tano inaonesha wazi kuwa inataka maendeleo ya haraka, lakini kuwa na maendeleo bila kuwa na dira na demokrasia ya kweli haiwezekani.
“Huwezi kusema uchumi umekuwa wakati wananchi ni maskini, ili uweze kusema kwamba uchumi umekuwa ni lazima uwe na watu ambao si maskini na wana uwezo wa kupata mahitaji yao ya lazima,” amesema.
“Tanzania hakuna dira tunaenda wapi? kumbuka mwanzoni kulikuwa na Azimio la Arusha hiyo ilikuwa ni dira ya kulifanya taifa kujua wapi linakwenda lakini kwa sasa tunayumba daraja kati ya maskini na matajiri ni kubwa mbaya zaidi wapo vijana wengi wenye elimu lakini hawana ajira.
“Juhudi zote nzuri za awamu ya tano bila kuwa na dira ni bure hata hivyo dira ya nchi inatokana na Katiba mpya ambayo inatokana na rasmu ya maoni ya wananchi ya Jaji Mstaafu Joseph Warioba na si vinginevyo,” amesema.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Jukwaa la Katiba Tanzania, Hebron Mwakagenda, amesema kuwa haiwezekani serikali ikatumia fedha za walipa kodi zaidi ya bilioni 100 kwa ajili ya mchakato wa katiba halafu isipatikane.
Amesema Jukwaa la Katiba ya Tanzania ,ni kuhakikisha inawaamsha Watanzania pamoja na Asasi mbalimbali ili kudai katiba ya wananchi ambayo inatokana na maoni yao.
Katika hatua nyingine Mwakagenda amesema jukwaa hilo limemwandikia barua nne rais John Magufuli, lakini hajajibu hata moja hadi leo.
Leave a comment