JESHI la Polisi nchini limetangaza msako wa kuwakamata na kuwadhibiti waganga wa tiba asili wanaojihusisha na vitendo vya upigaji wa ramli chonganishi zinazochangia kuwepo kwa mauaji ya watu hapa nchini. Anaripoti Moses Mseti, Magu … (endelea).
Msako huo umetangazwa ikiwa ni siku chache tangu kutokea kwa mauaji ya watoto wadogo na vikongwe katika mikoa ya Njombe na Simiyu yanayohusishwa na imani potovu za kishirikina
Msako huo umetangazwa leo na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Simon Sirro wakati akizungumza na kamati ya ulinzi na usalama na askari Polisi wa Wilaya za Magu na Kwimba mkoani Mwanza ikiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya kikazi katika mikoa ya kanda ya ziwa.
IGP Sirro, amesema jeshi la Polisi litaendelea kufanya misako ya mara jwa marao ili kuwabaini waganga wa tiba asili wanaofanya vitendo vya upigaji ramli chonganishi zinazosababisha kuendelea kuwepo kwa mauaji ya kutisha kwa raia, yanayotokana na imani potofu.
“Matatizo yaliopo simiyu (mkoa) hayana utofauti na Magu ni sawa kwa hiyo niwaonbe sana suala hili lazima tuwe na msako wa mara kwa mara na speed (kasi) ya hawa jamaa ni kubwa.
“Hawa jamaa wakiwa stable bila kuwa stabilize watatusumbua, muda wote ni kuwakamata ukiingia kwenye nyumba ya mganga wa kienyeji lazima utakuwa gorvement office (ofisi ya serikali) utakuta kuna mkia wa mende na vitu vingi,” amesema Sirro.
Amesema mipango ya jeshi hilo ni kuwasumbua waganga hao wasipate muda wa kutulia na kamata kamata hiyo itasaidia kupunguza tatizo la upigaji ramli chonganishi na vifo vitokanavyo na tatizo hilo.
Katika hatua nyingine IGP Sirro amewatama askari Polisi kuacha kujihusisha vitendo vya rushwa vinavyochangia kushusha heshima ya askari pamoja na kuwahimiza kupunguza vitendo vya uhalifu kwenye maeneo yao.
“Heshima yenu ni kupunguza uhalifu pamoja na rushwa na rushwa yenyewe ni shilingi elfu mbili na hizi ndogondogo, we have to change (lazima tubadilike).
“Askari akimuona mtu anakuja tu unafikiria pesa yake mfukoni utafikiri ulimsaidia kutafuta it’s going to cost you hii inaenda kukuumiza,” amesema Sirro.
Mkuu wa Wilaya ya Kwimba, Senyi Ngaga amesema katika kipindi cha Januari mpaka sasa kuna makosa 27 ya mimba za utotoni na kwamba pamoja na hilo bado kuna idadi kubwa ya watoto wanaobakwa.
“Ukiacha mimba za utotoni kuna watoto wengi ambao wanaobakwa kwa hiyo bado tunaendelea kuangalia sheria ichukue mkondo wake lakini inakuwa ni ngumu Sana,” amesema Ngaga.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Kwimba, Shanif Mansoor amesema ongezeko kubwa la mimba za utotoni katika maeneo mengi nchini linachangiwa na ukosefu wa elimu, hivyo, amehimiza kuendelea kutolewa kwa elimu kwenye jamii pamoja na mabinti wadogo.
Leave a comment