Saturday , 20 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Msajili ana ugomvi gani na Azaki?
Habari za SiasaMakala & UchambuziTangulizi

Msajili ana ugomvi gani na Azaki?

Spread the love

TAREHE 9 Agosti 2017, msajili wa asasi za kiraia alitoa maagizo kwa asasi za kiraia nchini kufanya kuhakiki wa uwepo wao. Uhakiki ulihusu uwasilishaji wa taarifa za msingi za asasi hizo, ikiwamoja Katiba, orodha za wanachama, taarifa za fedha na nyinginezo. Anaandika Mwandishi Wetu … (endelea). 

Msajili alitoa maagizo haya kwa sababu pamoja na kwamba alikuwepo kwenye idara husika kwa muda mrefu alikuwa hajui idadi ya asasi zilizopo nchini. Katika zoezi la uhakiki ilitegemewa kuwepo azaki zaidi ya 8,000 nchi nzima. Lakini zilizofanikiwa kujitokeza zilikuwa asasi 3, 186 tu.

Msajili huyo ambaye alifahamika sana kwenye asasi za kiraia kwa tabia yake ya kuzitishia kwa kuwabambikia makosa na kuwadai rushwa, alishindwa katika kipindi chake kuwa msaada mkubwa kwa sekta hiyo aliyoiongoza. 

Msajili huyo kwa kushirikiana na sekretarieti ya Baraza la taifa la NGOs, amekuwa mstari wa mbele kuwashutumu viongozi wa asasi za kiraia hasa za kimataifa na kutumia vitisho kujipatia pesa. Mara nyingi asasi hizo zimepokea vitisho kutokana na mapungufu kama ya kulipa ada, usajili ama uwasilishaji wa taarifa. 

Msajili alikuwa akitumia vitisho ikiwa ni pamoja na kutumia vyombo vya dola kuwaadhibu viongozi wa mashirika. Kwa asasi nyingi za nyumbani msajili alifahamika kuwa mnufaika mkubwa wa ada zilizolipwa na asasi hizo. 

Wengi ya waliowahi kufika ofisini kwake kwa ajili ya usajili, wanatambua kuwa ilikuwa ngumu mno kupata usajili bila kutoa hongo. Wapo wailorudishwa kwa kutotoa hongo kwa sababu zisizokuwa na mantiki kama “Msajili kutopenda jina linalopendekezwa na asasi husika.”

Baada ya maagizo ya Agosti 2017, mwezi Januari 2018, msajili aliagiza kuanza kwa mchakato wa kubadili sera ya asasi za kiraia ya mwaka 2001. 

Kwa mujibu ya maagizo yake, msajili alieleza kuwa nia ya marejeo hayo ya sera ni kuhuisha sera inayosimamia sekta ya asasi za kiraia na kuweza kuratibu usimamiaji wa sekta. Maongezi kati ya msajili na baadhi ya asasi husika yalithibitisha nia ya msajili hasa kuwa ni kuweza kuzidhbiti asasi za kiraia. 

Hii ni kutokana na malalamiko yaliyowasilishwa na Rais mara kadhaa mara nyingine mbele ya vyombo vya habari dhidi ya alichokiita “asasi za hovyo hovyo.” Alitoa kauli hiyo, alipozungumza mjini Bagamoyo tarehe 22 Juni 2017, kuhusu asasi zilizotetea haki ya wasichana kurudi shuleni wanapopata mimba. 

Tarehe 12 Septemba 2018, rais John Magufuli, alimuagiza katibu mkuu mteule wa wizara ya maendeleo ya Jamii kwenda kushughulikia NGOs. Rais alilalamika kile alichokiita, “NGOs nyingi hazina transparency (uwazi).” Akaongeza, “uende wewe pale, ukashulikie usajili wa hizi asasi.”

Muswada ulioletwa bungeni bila shaka ni juhudi za katibu mkuu huyo mteule kushughulikia malalamiko ya rais. Inafahamika kuwa mteule huyo wa rais ni mbobezi wa sayansi ya siasa akitokea chuo kikuu cha Dar es Salaam ambako kwa muda alikuwa akitoa mapendekezo kwa rais kuhusu udhibiti wa asasi za kiraia.

Kiongozi huyo wa umma ambaye anafahamika kuwa mwanachama mwaminifu na kiongozi wa Chama Cha Mapinduzi mkoani Singida, alifanikiwa kumuaminisha rais kuwa ni rahisi kudhibiti asasi za kiraia kwa kutumia sheria.

Kinachotatiza katika mapendekezo yanayopendekezwa kwa mabailiko haya ni kuwa wengi wasiotarajiwa wataathirika. Zilipoanza juhudi za awali kupitia tamko la katibu mkuu huyo la mwezi Septemba 2018, kuzitaka asasi zote kujisajili chini ya sheria ya NGOs, asasi kadhaa ziligoma kufanya hivo. 

Baadhi ya asasi hizo zilimueleza bayana katibu mkuu huyo na msajili mpya kuwa hakukuwa na sababu ya msingi kulazimisha asasi kuhamia kwenye usajili mpya kwani asasi hizo zipo kwa mujibu wa sheria. 

Asasi nyingi pamoja na kutosajiliwa kama NGO zimekuwa zikitimiza masharti mengi hata zaidi ya yale yanayohitajika kwenye sheria. Katika kuthibitisha hilo asasi hizo zimenufaika mno na fedha za wahisani kwa kupokea na kutumia mamilioni ya dola za kimarekani. Ripoti za asasi hizo zipo kwenye mitandao hata kabla ya kudaiwa na asai.

Msajili kutokana na nongwa, ameleta sheria itakayolazimisha mpaka makanisa kutawaliwa naye. Hata kampuni za binafsi sasa zinaweza kufutika kwa chafya ya msajili. Hakuna bodi za wadhamini zitabaki salama kwa mapendekezo haya. Yani leo hii bodi ya hospitali ya TMJ inaweza ikajikuta imefutwa tu! 

Kwa mabadiliko haya ya sheria, Ibara ya 74 bodi ya wadhamani ni uhusiano wa Kisheria wa kusimamia mali. Kwa ilivyo sasa bodi nyingi kama ya hospitali ya TMJ, Aga Khan, Hindu Mandal zinasimamiwa na kuendeshwa na bodi za wadhamini. Msajli anataka wadhamini wasifanye biashara ya aina yeyote bali wasimamie tu mali kwa mujibu wa mahusiano ya Kisheria. 

Msajili na maboss zake wana hasira na NGOs mpaka wanataka kuyafuta makampuni. Kwa kuwa asasi kadhaa zimejisajili kama kampuni zisizotengeneza faida, msajili amekwenda kuvamia madaraka ya usimamizi wa kampuni. 

Katika kutimiza adhma hiyo, msajili amefikia hatua ya kubadili hata maana ya kampuni na kutunga maana mpya ambayo haijwahi kutokea duniani. Dunia nzima inajulikana kuwa kampuni ni kikundi ama chombo chenye uhai wa Kisheria kutimiza malengo fulani.

Msajili wa Tanzania ameamua kuwa hapa nchini kampuni ni chombo “kinachofanya biashara tena mahususi ya ama uwekezaji, ununuzi na uuzaji.”

Hii ni hatari kubwa kwa sababu tutakuwa kisiwa ambacho waliowahi kuendesha kampuni kwingine duniani hawezi kufanya hivyo nchini. Kwa mapendekezo ya mabadiliko ya sheria, msajili anaweza tu kuamua kufuta kampuni bila kujali jitihada ama uwekezaji uliowekwa na wahusika. 

Ikitokea mmoja wa waanzilishi wa kampuni husika amezuiwa kuingiwa nchini basi ndio mwisho wa kampuni! Shule  nyingi ya binafsi zimesajiliwa kama kampuni zisizotengeneza faida. Kwa hasira hizi za msajili, shule hizo nyingi zijiandae kufutwa!

Msajili anataka ili kulinda uonevu wake na kwa kutaka kuagiza vyombo vya dola kusimamia asasi za kiraia. Ibara ya 27 ya muswada, msajili kupewa mamlaka ya kuagiza vyombo vya dola kushughulikia asasi. 

Yani asasi haijapeleka ripoti ama haijtangaza wahisani ama isingiziwe kula au kutoa rushwa ipelekewe vyombo vya dola labda polisi na jeshi ili impe msajili ushahidi! Sasa msajili anakuwa na mamlaka kuliko mwenyekiti wa wilaya au mkoa wa Kamati ya Ulinzi na Usalama? Msajili huyu huyu ambaye huko awali aliwaonea asasi mbalimbali? Hii si sawa na chizi kupewa rungu?

Msajili na wanaomtuma waache hasira!

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Dk. Mwakyembe : Zanzibar waliongoza kutaka Serikali 2 za muungano

Spread the love  MWANASIASA mkongwe nchini, Dk. Harrison Mwakyembe, amesema mjadala wa...

Habari za SiasaTangulizi

Rais Samia ataja mikakati ya kufikia trilioni 2 biashara Uturuki, Tz

Spread the loveWakati Tanzania na Uturuki zikidhamiria kuongeza kiwango cha biashara hadi...

BiasharaHabari za Siasa

Mavunde aagiza Perseus kuharakisha fidia Sengerema

Spread the loveWaziri wa Madini, Anthony Mavunde ameipongeza Kampuni ya Perseus kwa...

Habari za Siasa

Kigogo Chadema awanyooshea vidole vigogo serikalini kuhusu ripoti ya CAG

Spread the love  MWANACHAMA wa Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Boniface Jacob, amedai...

error: Content is protected !!