KAMATI ya uendeshaji na usimamizi wa Ligi (kamati ya Saa 72) imemfungia michezo mitatu mchezaji wa klabu ya Simba, Bernad Morrison na kumpiga faini ya Tsh. 500,000 mara baada ya kumpiga ngumi beki wa Ruvu Shooting, Juma Nyosso. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Morrison alifanya tukio hilo kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ambao Simba walipoteza kwa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Kwa mantiki hiyo mchezaji huyo atatumikia adhabu hiyo kuanzia mchezo ujao dhidi ya Mwadui FC siku ya Jumapili mpaka mchezo wa watani wa jadi utakao wakutanisha Simba na Yanga tarehe 7 Novemba, 2020.
Aidha kamati hiyo pia imemfungia michezo mitatu beki wa Ruvu Shooting, Juma Nyosso na kumtaka alipe faini ya Tsh. 500,000 mara baada ya kumkanyaga kwa makusudi mchezaji wa Simba, Bernard Morrison.
Kwenye mchezo huo huo pia kamati hiyo imemtoza faini ya Tsh. 500,000 na kumfungia michezo mitatu mchezaji wa Ruvu Shooting, Shabani Msala kwa kosa la kumpiga teke Bernard Morrison.
Adhabu hizo zote zimetolewa kwa kuzingatia kanuni ya 39(5) ya Ligi Kuu inayohusu uthibiti wa Wachezaji
Leave a comment