MWENYEKITI wa Halmashauri ya wilaya ya Morogoro, Kibena Kingu ameuomba Mradi wa kuleta mageuzi katika Sekta ya mkaa Tanzania (TTCS) usiwasahau katika awamu ya tatu ya mradi kufuatia mapato makubwa katika vijiji yanayozidi makusanyo ya mapato ya Halmashauri. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Kingu alisema hayo jana wakati akifungua mkutano wa waheshmiwa madiwani na wadau wa misitu uliofanyika mjini hapa ambapo alisema, kufuatia mradi huo kwa awamu ya pili kutakiwa kuisha mwezi Novemba mwaka huu ni vema Mradi ukaona umuhimu wa kuwakumbuka kuendeleza mradi.
Alisema, wilaya hiyo inaukubali mradi huo kutokana na kuwa wasimamizi wazuri wa misitu, kukomesha uvunaji holela na kufanya fedha za uvunaji endelevu wa misitu kuonekana hata katika matumizi mbalimbali ya maendeleo ya vijiji vyenye mradi tofauti na ilivyokuwa zamani.
Kingu alisema, kijiji cha Mlilingwa kimekuwa na uwezo wa kukusanya mapato ya Sh 160 milioni pekee fedha ambazo zinazidi makusanyo ya Halmashauri.
Alisema, mradi huo unauwezo mkubwa wa kusaidia katika maeneo ya vijiji vingi vyenye msitu badala ya msitu kuendelea kuharibiwa ambapo kwa sasa wametenga msitu mwingine katika kijiji cha Sesenga.
Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Shirika la kuhifadi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), Emmanuel Lyimo alisema, TFCG na Mtandao wa Jamii wa usimamizi wa Misitu Tanzania (MJUMITA) wana lengo la kusaidia usimamizi wa misitu kwenye vijiji kuwa endelevu na kuona wananchi wananufaika na misitu huku wakikabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.
Leave a comment