VIONGOZI mbalimbali wa umma wakiwamo Wabunge leo wamemiminika katika ofisi za Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kuwasilisha tamko kuhusu rasilimali na madeni huku Rais John Magufuli akitaka Desemba 31 mwaka huu iwe mwisho. Anaripoti Hamisi Mguta … (endelea).
Hata hivyo, wakati hayo yakifanyika leo, Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea (Chadema), amekosoa utaratibu unaotumika katika kupokea fomu hizo na kwamba hakuna sehemu yoyote ambayo anasaini mtumishi wa umma anapowasilisha fomu zake.
Kubenea akizungumza na MwanaHalisiOnline mchana huu, amesema kasoro nyingine ambayo ameiona ni kutotolewa elimu ya kutosha kuhusu jambo lenyewe kwa watumishi wa umma.
Aidha, amesema baadhi ya watumishi wa umma wanajadiliwa wanaposhindwa kuwasilisha fomu hizo ama kutenda makosa mbalimbali ya kimaadili, lakini wengine hawaguswi hata kama wakifanya makosa.
Alitoa mfano kwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ambaye alifikishwa katika Sekretarieti hiyo kwa kosa la kughushi vyeti vya elimu, lakini mpaka leo kesi yake inapigwa danadana.
Mfano mwingine amesema Sekretarieti hiyo imeshindwa kutenda haki ikiwamo kushindwa kuwashughulikia walioiba fedha za Escrow wakiwamo watumishi wa umma.
Kubenea amesema mambo hayo yanaifanya Sekretarieti kupoteza hadhi kwa kuwa haitendi haki kwa kila anayestahili na kwamba kuna upendeleo.
Juzi akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, mwenyekiti wa Sekretarieti hiyo, Jaji Mstaafu, Harold Nsekela, aliwataka viongozi wa umma kuwasilisha fomu zao.
Miongoni wa watumishi waliowasilisha fomu hizo mpaka leo mchana ni Rais John Magufuli.
Baada ya kuwasilisha fomu hizo, Rais Magufuli alimtaka Kamishna wa Sekretarieti hiyo kutopokea fomu ya kiongozi yoyote ambaye atakuwa hajawasilisha tamko lake ifikapo Dessemba 31, 2017.
“Mhe. Jaji Nsekela ikifika tarehe 31 Desemba, ambayo ni siku ya mwisho kwa Mujibu wa Sheria, weka mstari na usipokee fomu zingine, halafu tuone sheria itafanyaje, nakutakia kazi njema” alisisitiza, Rais Magufuli.
Tamko la viongozi wa umma kuhusu rasilimali na madeni linatolewa kwa mujibu wa kifungu cha 9 na cha 11 cha sheria ya maadili ya viongozi wa umma namba 13 ya mwaka 1995.
Leave a comment