WANANCHI wametakiwa kutoa taarifa pale wanapokutana na watu wenye dalili za magonjwa ya mlipuko, ikiwemo ugonjwa wa Ebola. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa na Francis Mbuya, Mhandisi Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wakati akikabidhi majengo ya kukabiliana na magonjwa ya mlipuko mkoani Mwanza.
“Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, imeendelea na jitihada za kuimarisha mikakati ya kudhibiti magonjwa ya milipuko ikiwemo Ebola na Kipindupindu, hivyo mnapomuhisi mtu kuwa na dalili, toeni taarifa,” amesema Mhandisi Mbuya.
Amesema, wizara hiyo imekuwa ikitekeleza ujenzi wa miradi mbalimbali ya ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma za afya katika hospitali za Rufaa na Kanda, lengo likuwa kupambana na magonjwa ya aina zote.
“Miradi hii imejengwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Hospitali ya Mawenzi mkoani Kilimanjaro na Buswelu, mkoani Mwanza, inalenga kupambana na magonjwa ya mlipuko ikiwemo Ebola na Kipindupindu.
“Miradi yote miwili (Buswelu Mwanza na Mawenzi Kilimanjaro) imegharimu jumla ya Sh. 2.2 Bilion kutoka Sh. 897 milion iliyotengwa kwa kila mradi. Hii ni kutokana na maboresho yaliyofanyika katika miradi hiyo, ili kuweza kutoa huduma bora kwa Wananchi,” amesema.
Leave a comment