OFISI ya Mkemia Mkuu wa Serikali imefanikiwa kutambua miili 50 kati ya 69 ya watu waliopoteza maisha katika ajali ya moto wa lori la mafuta mkoani Morogoro. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa jana tarehe 20 Agosti 2019 na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu wakati akizungumzia ziara ya Rais John Magufuli katika ofisi hiyo iliyoko jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika ziara hiyo, Rais Magufuli ametoa wito kwa ndugu kujitokeza ili wachukuliwe sampuli zao kwa ajili ya kutambua miili ya ndugu zao mahala ilipozikwa.
Aidha, Rais Magufuli ameitaka ofisi hiyo kuendelea kutoa taarifa kwa umma ili ziwafikie walengwa kitendo kitakachosaidia kupata ndugu wa miili 19 iliyobakia.
“Wale wengine kama alivyotoa wito kiongozo wenu basi kama kuna ndugu wanaweza kuwa tayari wapimwe, ili pawepo ‘comparison’ ya marehemu wachache waliobakia. Mmefanya kazi kubwa sana na hizi taarifa mzitoe mapema mzitangaze sababu itasaidia ndugu wa marehemu kupimwa,” amesema Rais Magufuli.
Wakati huo huo, Rais Magufuli amewaomba Watanzania kuwaombea kwa Mungu majeruhi wa ajali hiyo wanaopatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, ili wapone haraka na waungane na familia zao.
“Lakini wale walioko kule tuendelee kuwaombea Mungu awasaidie, kikubwa ninachotaka kusema ni kwamba ofisi yenu ya mkemia mkuu na ninyi wakemia mmefanya kazi kubwa sana ninawapongeza sana,” amesema Rais Magufuli.
Ajali ya moto wa lori la mafuta ilitokea tarehe 10 Agosti mwaka huu mkoani Morogoro, ambapo mpaka sasa imepoteza maisha ya watu zaidi ya 90.
Leave a comment