SERIKALI imeainisha mikakati mitano inayofanya katika kuwajengea uwezo waendesha bodaboda ukiwemo faida za kujiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo bungeni na Antony Mavunde, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Vijana, Kazi na Ajira wakati akijibu swali la msingi la Mbunge wa Lushoto, Shabani Shekilindi (CCM).
Katika swali hilo, mbunge huyo alisema uendeshaji bodaboda ni ajira kama zilivyo ajira nyingine nchini.
Amehoji, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea uwezo vijana hao ili kuifanya kazi yao hiyo iwe rasmi na yenye kutambulika kama kazi nyingine zozote.
Akifafanua Mavunde amesema, mipango hiyo ni pamoja na kutoa mafunzo ya udereva kupitia Jeshi la Polisi kwa waendesha bodaboda na hatimaye kupatiwa leseni za udereva.
Aidha, kama ilivyo vyombo vingine vinavyotoa huduma za usafiridhaji, usalama wa waendesha bodaboda na abiria umeendelea kusimamiwa na kulindwa wanapotekeleza majukumu yao barabarani.
Mwingine ni kuhamasisha uundwaji wa vikundi vya waendesha bodaboda ili hatimaye viweze kuwezeshwa kwa mitaji na mafunzo kupitia mifuko ya uwezeshaji wananchi kiuchumi na wadaiu wengine.
Aidha, kuwapatia maeneo ya kuegesha bodaboda ya kuyatambua pamoja na kuwapatia vitambulisho.
Pia, kuwapatia waendesha bodaboda mafunzo ya ujasiriamali na hatimaye kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu na kuwaunganisha na taasisi zingine zinazotoa mikopo.
Na kuwa, watapatiwa elimu juu ya faida za kujiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii pamoja na kuwaunganisha na mifuko husika.
Leave a comment