Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Mjumbe NEC ahoji wanaohamia CCM ‘kupewa shavu’, JPM amjibu 
Habari za Siasa

Mjumbe NEC ahoji wanaohamia CCM ‘kupewa shavu’, JPM amjibu 

Nsojo
Spread the love

MALALAMIKO ya wanasiasa wa upinzani wanaohamia Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuwazidi kete ‘wazawa’ katika fursa za uteuzi, yameibuliwa katika Mkutano wa Halmashauri Kuu ya chama hicho (NEC). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).

Malalamiko hayo yameibuliwa leo Ijumaa tarehe 10 Julai 2020 na Mjumbe wa NEC aliyejitambulisha kwa jina la Nsojo, kutoka mkoani Songwe, katika Mkutano wa halmashauri hiyo, uliofanyika  jijini Dodoma.

Mbele ya Mwenyekiti wa CCM, Rais John Pombe Magufuli, Nsojo amevunja ukimya kuhusu malalamiko hayo, akisema kwamba kitendo cha wageni kupewa kipaumbele kinawavunja moyo wazawa.

          Soma zaidi:-

“Kuna malalamiko ya Wanasongwe kwamba wanachama wa upinzani wanavyokuja kwetu ni neema, kama Katiba ya CCM inavyosema wote ni sawa.”

“Ni kweli tunawapokea lakini wananchi wamekuwa wakivunjika moyo wanavyopewa nafasi za uongozi katika chama chetu,” amesema Nsojo.

Nsojo amedai, wapo WanaCCM waliojitoa kwa hali na mali kukijenga chama hicho na hata wengine kuharibiwa mali zao katika harakati zao na kwamba kitendo cha fursa hizo kuwapita, hakileti taswira nzuri.

John Magufuli, Mwenyekiti wa CCM

“Tukiacha wanachama wenzetu ambao walipigana kufa na kupona 2010 na 2015, wengine hata kuharibiwa mali zao wanavunjika moyo. Baada ya kuona wanapita bila mbadala na viongozi wa CCM wa eneo husika wanaunga mkono kwa asilimia nyingi kama Tunduma na Momba,” amesema Nsojo.

Akijibu malalamiko hayo, Rais Magufuli amweleza mjumbe huyo wa NEC kwamba, yeye peke yake ndio hawataki wageni, lakini CCM inawahitaji.

“Haya nimekusikia, nilifikiri hilo ungezungumzia huko huko kwenye vikao vyako kwenye  kamati ya siasa ya wilaya na ya mkoa, kwamba wanaokuja kule huwahitaji wewe lakini chama hiki ni cha watu kina misingi yake kinameza watu wote,” amejibu Rais Magufuli.

Hata hivyo, amemshauri Nsojo kwamba, malalamiko hayo anatakiwa ayawasilishe katika vikao vya Kamati za Siasa ya CCM za wilaya au mikoa, kwa ajili ya kutafuta ufumbuzi.

Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC)

“Kwa hiyo hilo suala kama liko kule mkalizungumzie kwenye kamati ya siasa mkalitafutie ufumbuzi,  tunao watu wengi walikuwa vyama vingine lakini sasa hivi ni  CCM damu damu,” amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli amewataka WanaCCM kuvumiliana kwa kuwa chama hicho kinapokea watu wote, ambao wako tayari kufuata maadili na misingi yake.

“Saa nyingine lazima tuwe na mioyo ya kuvumiliana na kumtanguliza Mungu, chama hiki kinapokea wote ilimradi wanazingatia masharti ya chama,” amesema Rais Magufuli.

Akifafanua kuhusu wageni kuteuliwa katika masuala mbalimbali, Mwenyekiti huyo wa CCM amesema, wanapitishwa kwa kuwa wanaushawishi kwa wananchi, kuliko wazawa.

“Inawezekana huyo aliyekuja mna wasiwasi atawashinda ndio maana amekuwa anawashinda kila mara (wakiwa upinzani), sababu mngekuwa mnawashinda.  Sasa kama alikuwa anawatandika na akipigiwa kura za maoni akashinda, atachaguliwa na kupigiwa kura za wananchi,” amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli amesema, wageni wamekuwa wanashinda katika chaguzi wakiwa upinzani, ikilinganishwa na wagombea wanaopitishwa na CCM.

“Tatizo moja la siasa zetu, tunajiwekea vizingiti kwamba akija huyu atashinda, lakini mkiachiwa ninyi hamshindi nafikiri meseji mmeipata. Sasa mkiingia kwenye group (makundi) zenu mkaanza kujibishana amerudishwa huyu.

Amerudishwa kwa misingi kwamba mlimzuia njia akapitia dirishani, amerudi kupitia mlangoni mnataka mumzuie? muwe na uvumilivu,” amesema Rais Magufuli.

Mwenyekiti huyo wa CCM amefafanua zaidi, “Tena mimi ningetaka aliyeingia aendele kushinda siku moja awe mjumbe wa NEC, kwani mwanamke akikosea au mme wako, siku nyingine akakuomba msamaha utakataa? si ajabu akaja na mapenzi mazuri kuliko ya zamani. Amejifunza huko mbinu nyingi na mbaala unakataa uhondo huo?”

Desturi ya wanasiasa wa upinzani wanaojiunga na CCM kupewa nyadhifa mbalimbali serikalini na katika vyombo vya uongozi wa kisiasa, imeonekana katika nyakati mbalimbali, ambapo wapo walioteuliwa kuwa wakuu wa wilaya, makatibu tawala.

Na hata wengine kupitishwa kuwa wagombea wa CCM katika chaguzi mbalimbali, ikiwemo chaguzi ndogo zilizofanyika baada ya waliokuwa wabunge na madiwani wa upinzani kujiuzulu kisha kujiunga na CCM na kuteuliwa tena kuwa wagombea wa chama hicho, katika maeneo yao waliojiuzulu wakiwa wapinzani.

Mwita Waitara, ni miongoni mwa wanasiasa wa upinzani waliokula shavu baada ya kurudi CCM, kabla ya kujiunga na chama hicho tawala alikuwa Mbunge wa Ukonga kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema.

Alipong’atuka aliteuliwa tena na CCM kugombea jimbo hilo na kufanikiwa kulirejesha mikononi mwake.

 

Baada ya kushinda katika uchaguzi mdogo huo, Waitara aliteuliwa na Rais Magufuli kuwa Naibu Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI.

David Kafulila, aliyekuwa mwanachama wa Chadema alipojiunga CCM, aliteuliwa kuwa Katibu Tawala mkoani Songwe, huku Patrobas Katambi, aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha) aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, baada ya kujiunga na CCM.

Julius Mtatiro, aliyekuwa Kiongozi wa Kamati ya Uongozi ya Chama cha Wananchi (CUF), baada ya kujiunga na CCM, aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma pamoja na Moses Machali aliyetoka NCCR-mageuzi na kujiunga na CCM, aliteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Nanyumbu Mkoa wa Mtwara.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

Habari za SiasaTangulizi

Mashirika matano yapata hasara mabilioni ya fedha

Spread the loveMASHIRIKA matano ya Serikali yanayojiendesha kibiashara, yamepata hasara ya mabilioni...

error: Content is protected !!