TUKIO la Irene Uwoya, Msanii wa Filamu nchini kuwamwagia fedha waandishi wa habari, limelaaniwa na Taasisi ya Vyombo ya Habari Kusini mwa Afrika (MISA) tawi la Tanzania. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Kupitia tamko lake ililotoa leo tarehe 16 Julai 2019, MISA Tanzania imeeleza kwamba, limedhalilisha tasnia ya habari pamoja na kukebehi fedha ya Tanzania.
“Taaluma ya habari kama zilivyo taaluma nyingine inapaswa kulindwa, kuheshimiwa na kuenziwa na siyo yeyote kuisigina kwa kuwa ameamua kufanya hivyo kutokana na mamlaka, umaarufu, uwezo wa kifedha na nguvu nyinginezo zozote,” inaeleza sehemu ya tamko la MISA Tanzania na kuongeza.
“Wanahabari wanapaswa kuelewa wao ndiyo walinzi wa taaluma yao na kutoa taswira njema, itakayolinda taaluma na utu wao kwa ujumla, wanapaswa kukataa kwa namna yoyote udhalilishwaji ambao utashusha hadhi ya mmoja mmoja na tasnia kwa ujumla wake,”
Taasisi hiyo imeeleza kuwa, kitendo hicho ni kosa la jinai kwa mujibu wa kifungu namba 332A cha kanuni ya adhabu (Penal Code) sura ya 16 kama ilivyorejewa mwaka 2002.
“Sheria ya fedha hairuhusu kukebehi fedha ya nchi kwa namna yoyote ile kwa kuwa ndiyo utambulisho wa taifa na tunu yetu,” imeeleza tamko la MISA Tanzania.
MISA Tanzania imetoa wito kwa mamlaka husika kuhakikisha kwamba tukio kama hilo lisijirudie tena.
“MISA Tanzania inalaani vitendo hivi na kutaka visijirudie tena, pia inaamini mikutano kama hiyo licha ya kuhudhuriwa na wandishi wa habari wapo pia watu wasio wanahabari ambao huingia kuchukua picha kwa sababu zao binafsi.”
Jana tarehe 15 Julai 2019 katika mkutano wa wasanii wa filamu Tanzania na wanahabari uliofanyika jijini Dar es Salaam, Uwoya alimwaga fedha kama njugu kwa wanahabari, ambapo waliowengi walikanyaga kuziokota fedha hizo.
Leave a comment