MIMBA na ndoa katika umri mdogo bado vinaitesa wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma, ingawa serikali haina takwimu sahihi za wasichana wanaokumbwa na matatizo hayo wakaiwa na umri mdogo, anaandika Dany Tibason.
Ofisa Maendeleo ya Jamii wa wilaya ya Chamwino, Sophia Swai, amesema juhudi zinafanyika kupata takwimu hizo ili kutengeneza mkakati wa kupambana nazo.
Swai ametoa kauli hiyo juzi wakati wa mafunzo kwa wadau wanaopinga ndoa za utotoni na mpango wa kupunguza mimba katika umri mdogo ambayo yalifanyika katika kijiji cha Nzali wilayani Chamwino.
Mafunzo hayo yaliratibiwa na Shirika lisilokuwa la kiserikali la WOWAP kwa ufadhiri wa Foundation for Civil Society (FCS) na washiriki walitoka kata sita za Manchali, Chilonwa, Msanga, Mpwayungu, Mlowa barabarani na Mlowa Bwawani.
Swai alitaja sababu za serikali kukosekana kwa takwimu sahihi ni uhaba wa fedha katika bajeti za halmashauri ambazo zingeweza kusaidia idara ya Maendeleo kufika kila maeneo kwa ajili ya kuchukua taarifa na kutoa elimu.
Sababu nyingine ni mpangilio usiokuwa jumuishi ndani ya serikali kwani kila idara inafanya kazi na kupeleka taarifa mahali inapotakiwa bila ya kuzifanyia majumuisho.
“Kwa mfano, elimu, dawati la jinsia polisi,, ustawi wa jamii na sisi maendeleo ya jamii tunafanya kazi hiyo kupinga ndoa za utoto na kutoa elimu ya mimba za utotoni, lakini wote tunapeleka ripoti kwa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hapo kuna shida maana wengine wanapeleka taarifa zilizopitwa na wakati,” amesema Swai.
Amewanyooshea vidole wanasiasa kwamba wamekuwa wakivuruga taratibu nyingi za kitaalamu kwani wanaingilia mambo mengi na badala ya kusaidia wao wanasimama upande wa pili.
Mratibu wa mafunzo na mradi huo, Nasra Suleiman amesema mafunzo hayo yamesaidia kwa kiasi kikubwa katika mapambano ya ndoa za utotoni kwani hali ilikuwa ni mbaya katika wilaya hiyo.
Amekiri kuwa hivi sasa jamii imejitambua na wengi wameanza kuogopa kwani kila maeneo kumekuwa na watu wanaoweza kuzungumza hadharani kuhusu madhara ya ndoa za utotoni na hata kuisaidia serikali katika kuwafichua wahusika.
Kiongozi wa waendesha bodaboda kata ya Manchali, Onesmo Ndulani amesema tangu kuanza kwa mafunzo hayo wamekuwa na uelewa mpana ikiwemo kuzungumza na wenzao ambao wamekuwa na tabia ya ukware kwa watoto wa shule.
Ndulani amesema kata yao ina waendesha bodaboda wengi, lakini wamekuwa wakitumia mtindo wa kuwaelimisha hata abiria wanaowabeba huku wakiwekeana yamini ya kuwalinda watoto wa kike.
Leave a comment