UKATILI wa kijinsia dhidi ya watoto, umeongezeka kwa asilimia 7.7 kutoka matukio 13,457 mwaka 2017 hadi 14,419 mwaka 2018 huku mikoa mitano ikiongoza. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 4 Septemba 2019 na Dk. Faustine Ndugulile, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wakati akijibu maswali ya Goodluck Mlinga, Mbunge wa Ulanga, bungeni jijini Dodoma.
Katika maswali yake, Mlinga alihoji kama serikali imefanya utafiti kujua hali ya matukio ya ukatili wa kijinsia, huku akisema kwamba idadi ya kesi zinazofunguliwa mahakamani kuhusiana na ukatili huo ni ndogo ukilinganisha na ukubwa wa matukio hayo.
Akijibu maswali hayo, Dk. Ndugulile amesema Mkoa wa Tanga unaongoza kwa kuwa na matukio 1, 039 ukifuatiwa na mkoa wa Mbeya wenye matukio 1,001, Mwanza (809), Arusha (792), Tabora (618).
Dk. Ndugulile amesema kwa mujibu wa taarifa za Jeshi la Polisi kuhusu makosa ya ukatili wa kijinsia kwa watoto kwa mwaka 2018, vitendo vya ubakaji viliongoza kutikisa katika mwaka huo kwa kuwa na matukio 5,557, ikifuatiwa na mimba za utotoni (2,692), ulawiti (1,159), shambulio (965) na kujeruhi (705).
“Ni kweli kumekuwa na ongezeko la vitendo vya ukatili hasa ubakaji wa watoto na viokongwe, kwa mujibu wa taraifa za jeshi la polisi za mwaka 2018 za makosa ya ukatili wa kijinsia kwa watoto hali ya vitendo hivyo vimeongezeka,” amesema Dk. Ndugulile.
Kuhusu idadi ndogo ya kesi za ukatili wa kijinsia mahakani ukilinganisha na ukubwa wa matukio, Dk. Ndugulile amesema serikali inakabiliana na changamoto ya kuwachukulia hatua wahusika wa matukio hayo kwa kuwa wahusika wengi uharibu ushahidi.
Dk. Ndugulile amesema asilimia kubwa ya wanaohusika na ukatili huo ni wanafamilia, hivyo walengwa humalizana katika vikao vya kifamilia.
“Ni kweli matukio haya yanaongezeka, na changamoto ni asilimia zaidi ya 60 ya matukio haya yanafanywa na watu walio karibu na familia.
“Na tumekuwa tukipata changamoto kama serikali kuchukua hatua kwa wahusika sababu ndugu na jamaa wanakaa vikao vya familia wanaamua kumalizana kwa kutozana faini au kumtorosha mhusika,” amesema Dk. Ndugulile na kuongeza;
“Nitoe rai kwa jamii haya mambo hayawezi hayamalizwi katika mazingira ya majumbani badala yake waruhusu mkondo wa sheria uchukue hatua.”
Leave a comment