WIZARA ya Mambo ya Ndani ya Nchi imesema gharama za chakula kwa mfungwa mmoja kwa siku ni wastani wa shilingi 1,342. Anaripoti Dany Tibason … (endelea).
Hayo yalielezwa leo bungeni na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamadi Masauni alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Njombe Mjini, Edward Mwalongo (CCM).
Katika swali hilo Mwalongo alitaka kujua Serikali inatumia kiasi cha shilingi ngapi kuhudumia mfungwa mmoja kwa siku kwa ajili ya chakula.
“Vitendo kama kulala chini, kulala bila blanketi au shuka vimekuwa vya kawaida kabisa katika Magereza yetu. Je hii nayo ni sehemu ya adhabu ambayo wafungwa wanapewa kwa mujibu wa sheria,” alihoji Mbunge huyo.
Akijibu, Masauni amesema Jeshi la Magereza katika kutekeleza majukumu yake pia hutoa huduma ya chakula kwa wahalifu kupitia bajeti iliyotengwa na Serikali kila mwaka wa fedha.
Naibu Waziri huyo amesema gharama za chakula kwa mfungwa mmoja kwa siku ni wastani wa shilingi 1,342.
Amesema Serikali imeendelea kuboresha huduma za wafungwa na mahabusu kwa kununua vifaa mbalimbali vya malazi ikiwemo, magodoro shuka, mablanketi na madawa ya kuua wadudu.
Leave a comment