JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar ss Salaam linamshikilia Mfanyabiashara Kageta Kageta (35) mkazi wa Tabata Kinyerezi, kwa kosa la kukutwa na dawa za kulevya aina ya Heroin zenye uzito wa Gram 815.3. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 26 Oktoba 2018, Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Rebaratus Sabas amesema baada ya polisi kufanya upekuzi nyumbani kwake, walikuta madawa hayo yakiwa yamefichwa kwenye kontena ndani ya choo.
“Baada ya ufuatiliaji tuliweza kumtia mbaroni mtu huyo anayetuhumiwa kujihusisha na matukio hayo ya kihalifu, baada ya kumkamata na kumpekua aliweza kukutwa na madawa ya kulevya aina ya heroin, madawa hayo alikuwa ameficha eneo la chooni na kuyaweka kwenye kontena, na baada ya kumhoji alikiri kujihusisha na biashara hiyo muda mrefu,” amesema Kamanda Sabas.
Kamanda Sabas ameeleza kuwa, Jeshi la Polisi litamfikisha mahakamani mtuhumiwa huyo pindi uchunguzi ukikamilika.
“Anajinufaisha kwa biashara hii haramu ambayo inateketeza kizazi chetu cha kitanzania, nguvu kazi yetu inaharibika kwa yeye kufanya baishara zisizo halali. Jeshi la Polisi tutaendelea kuwatafuta wengine,” amesema Kamanda Sabas.
Leave a comment