MAHAKAMA ya Mkoa wa Iringa, imetupilia mbali ombi la Alex Kimbe, Meya wa Manispaa ya Iringa la kuzuia mchakato wa kumng’oa madarakani. Anaripoti Mwandishi Wetu, Iringa…(endelea).
Uamuzi huo umetolewa leo tarehe 27 Machi 2020 na mahakama hiyo mbele ya Aden Kanje, Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo.
Akitoa uamuzi huo, Hakimu Kanje amesema, ombi hilo limetupwa kutokana na kuwa na makosa, kitendo kilichopelekea mahakama hiyo kushindwa kusikiliza kesi hiyo kwa mujibu wa sheria.
Awali kikao cha kuendesha mchakato wa kumng’oa Meya Kimbe jana tarehe 26 Machi 2020, kilikwama baada ya madiwani wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kutohudhuria.
Hata hivyo, Hamid Njovu, Mkurugenzi wa Halmshauri ya Manispaa ya Iringa, ameitisha Mkutano Maalumu wa Baraza la Madiwani la manispaa hiyo, kesho tarehe 28 Machi 2020.
Miongoni mwa ajenda ya kikao hicho kesho, ni kupiga kura ya kutokuwa na imani na Meya Kimbe.
Leave a comment