BERNARD Kamilius Membe, Waziri wa zamani wa Mambo ya Nje nchini Tanzania amekubali ombi la wanachama wa ACT-Wazalendo la kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi, Dar es Salaam…(endelea)
Membe ametoa kauli hiyo leo Ijumaa tarehe 17 Julai 2020 ikiwa ni siku moja kupita tangu alipopokelewa rasmi ndani ya ACT-Wazalendo jana Alhamisi katika ukumbi wa Mlimani City Dar es Salaam.
Mwanasiasa huyo amejiunga na chama hicho cha upinzani baada ya kufukuzwa ndani ya chama tawala Chama Cha Mapinduzi (CCM) alichokulia kwa kile kilichoelezwa hakuwa na mienendo inayoridhisha tangu mwaka 2014.
Baada ya kupokelewa na wanachama pamoja na viongozi waandamizi wa ACT-Wazalendo wakiongozwa na Maalim Seif Sharif Hamad, Kiongozi wa chama hicho, Zitto Kabwe, mwanasiasa huyo aliombwa agombee urais.
Maalim Seif ambaye amekwisha kuchuklua na kurejesha fomu ya kuwania urais Zanizbar alisema, wanachama wa chama hicho wamemtuma amweleze Membe agombee urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Soma zaidi hapa
Maalim Seif: Membe unaogopwa, gombea urais Tanzania
Leo Ijumaa tarehe 17 Julai 2020, kupitia akaunti yake ya kijamii ya Twitter, Membe ameandika, “jana niliombwa na leo nimekubali rasmi kugombea nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia tiketi ya chama cha ACT Wazalendo.”
Jana niliombwa na leo nimekubali rasmi kugombea nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia tiketi ya chama cha ACT Wazalendo. Huu ni wakati muafaka kwangu wa kushiriki katika mazungumzo na vyama vingine kama Chadema ili tusimamishe "KISIKI CHA MPINGO" kimoja!
— Bernard K. Membe (@BenMembe) July 17, 2020
“Huu ni wakati muafaka kwangu wa kushiriki katika mazungumzo na vyama vingine kama Chadema ili tusimamishe “KISIKI CHA MPINGO” kimoja!.”
Katika mazungumzo yake jana baada ya kupokelewa, Membe aliomba kambi rasmi ya upinzani inayoundwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuungana katika uchaguzi huo ili kuhakikisha wanaiondoa madarakani serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu ujao.
Soma zaidi hapa
Membe akoleza moto urais Tanzania, atoa ombi Chadema
MwanaHALISI Online limezungumza na Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu kuhusu ambaye amesema kuna uwezekano Membe akachukua fomu ya kuwania urais leo Ijumaa.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari zaidi
Walitangulia kabla yake lakini wenyewe wamesalim amri anataka kujizalilisha tu hawa ndio wanaotamaa Na madaraka sio uongozi hawana lolote kama wewe no basi ni no hata kama utachinja bahari haitafaa kitu au umwetumwa kukiua hicho chama basi hogera na nyie wa vyama kueni na upeo kila uchaguzi mnarubuniwa na nyinyi hamusoni mtaburuzwa mpaka ? Ifikapo mwaka 2025 tutahamia chama nanihino?