WAZIRI wa zamani wa mambo ya nje na mahusiano ya kimataifa nchini Tanzania, Benard Membe amesema, anasubiri kwa hamu, barua ya wito ya kumtaka kufika kwenye Kamati ya Maadili na Usalama ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Akiandika katika ukurasa wake wa twitter, siku moja baada ya chama chake hicho, kutoa taarifa kuwa anapaswa kufika kwenye kamati ya Maadili, Membe amesema, “…nasubiri kwa hamu barua ya wito.”
Anasema, “kutokana na wingi wa meseji, nashindwa kumjibu kila mtu aliyeniandikia ujumbe kuhusu tangazo la kuitwa kwangu. Niseme tu kwamba, nasubiri kwa hamu barua ya wito.”
Kutokana na wingi wa messages, nashindwa kumjibu kila mtu aliyeniandikia ujumbe kuhusu tangazo la kuitwa kwangu kwenye Kamati ya maadili. Niseme tu kwamba; Nasubiri kwa hamu barua ya wito! Nitakwenda! Hoja zitatolewa na hoja zitapanguliwa. Stay tuned!
— Bernard K. Membe (@BenMembe) December 14, 2019
Katika taarifa yake ya kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana, tarehe 13 Desemba 2019 na Katibu wa Halmashauri Kuu ya taifa (NEC), Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole, CCM kimeeeleza kuwa viongozi wake watatu wandamizi, “watahojiwa” na kamati yake ya maadili na usalama.
Polepole amewataja viongozi wanaopaswa kuhojiwa na kamati hiyo, kuwa ni Membe, Kanal Abdulrahaman Kinana na Luteni Yusuf Makamba.
Kinana na Makamba, waliwahi kwa nyakati tofauti, kushikilia wadhifa wa ukatibu mkuu ndani ya chama hicho, huku Membe akiwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa.
Alisema, viongozi hao wandamizi, wataitwa mbele ya kamati hiyo, kujibu tuhuma za kimaadili zinazowakabili.
Membe, Kinana na Makamba, wamenukuliwa wakiutuhumu uongozi wa juu wa chama chao, kumkumbatia
Katika kinachoitwa, “kuvuja kwa mazungumzo yao waliyofanya kwa njia ya simu,” Membe, Makamba, Kinana, Nape Nnauye na January Makamba, kwa nyakati mbalimbali, walisikika wakimtuhumu Rais John Magufuli, kumkumbatia Cyprian Musiba, anayetukuna na kusingizia watu kadhaa mambo mbalimbali.
Kinana na Makamba, waliamua kufikisha malalamiko yao kwa Pius Msekwa, katibu wa kamati ya wazee ya chama hicho.
Katika barua yao kwa Msekwa, Makamba na Kinana wanasema, “vitendo vya Musiba, anayeonekana ametumwa na anayetumia mwamvuli wa CCM na Ikulu, kushambulia kila mtu, vinakidhalilisha chama chetu.”
Akiandika kwa kujiamini, kujibu madai hayo ya Polepole yanayomtaka kufika kwenye kamati ya maadili, Membe anasema, “…nasubiri kwa hamu sana barua ya wito. Nitakwenda; hoja zitatolewa na hoja zitapanguliwa.”
Jina la Membe – mwanadipromasia mashuhuri nchini aliyepata kuwa waziri wa mambo ya nje kwa miaka takribani nane ya utawala wa Jakaya Kikwete – limepata umaarufu mkubwa katika siku za karibuni, kufuatia kuhusishwa na mbio za urais katika uchaguzi mkuu wa 2020 kupitia CC.
Hata hivyo, Membe mwenyewe hajaweka wazi jambo hilo, ingawa watu waliokaribu naye wanasema, “ni lazima atajitosa kwenye kinyanganyiro hicho.”
Leave a comment