ALIYEPATA kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, katika utawala wa Jakaya Mrisho Kikwete, Bernard Membe, amemburuza mahakamani Cyprian Musiba. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Membe amefungua kesi hiyo mahakama kuu Kanda ya Dar es Salaam, akimtaka Musiba alipe fidia ya Sh. 10 bilioni kutokana na kumchafua jina lake.
Kesi hiyo ambayo imepewa Na. 220 ya mwaka 2018, imesajiliwa mahakamani wiki iliyopita.
Mbali na Musiba, mwanadiplomasia huyo mashuhuri nchini, amewashitaki pia mhariri wa gazeti la Tanzanite, na wachapishaji wa gazeti hilo.
Katika shauri hilo, Membe anawakilishwa na kampuni ya Millennium Law Chambers ya Dar es Salaam.
Musiba, ambaye amekuwa anajiita mwanaharakati anayejitegemea amekuwa mtetezi mkubwa wa serikali ya Rais John Magufuli na rais mwenyewe.
Musiba anashitakiwa kwa kutoa matusi dhidi ya Membe na kumtuhumu kuwa anamhujumu Rais Magufuli.
Anadai kuwa Membe amejipanga kugombea urais mwaka 2020, kumgombanisha rais na nchi wahisani na kushirikiana na maadui wa nchi kudhoofisha serikali.
Leave a comment