HALIMA James Mdee, Mbunge wa Jimbo la Kawe kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), amesema kauli ya Job Ndugai kwamba wabunge waliopewa adhabu hawatarudi bungeni hata wakienda mahakamani ni ya kupuuzwa, anaandika Irene Emmanuel.
Mdee ambaye pia ni mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha) amesema Ndugai amekuwa akiliendesha Bunge kwa upendeleo wa wazi, huku wabunge wa chama tawala wakiwa hawachukuliwa hatua wanapokosea.
Akizungumza, katika mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika makao makuu ya Chadema, jijini Dar es salaam Mdee amesema, “Ndugai anatapatapa na hivyo mimi nitaendelea kumpuuza, kama ambavyo nimekua nikimpuuza.
“Mahakama inafanya kazi yake, na endapo malalamiko yangu yakionekana hayana mantiki basi nitaendelea kutumikia adhabu niliyopewa.”
Itakumbukwa kuwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilitoa uamuzi wa kuwafungia Mdee na Esther Bulaya, Mbunge wa Bunda Mjini kuhudhuria vikao vya bunge kwa kipindi cha mwaka mmoja kutokana na kile kilichotajwa kuwa ni utovu wa nidhamu ndani ya bunge.
Hata hivyo, Mdee ameiambia MwanaHALISI online, “sisi tumeenda kudai haki yetu kupitia Mahakama Kuu, ambayo imepewa mamlaka yasiyo na kikomo kushughulikia masuala ya kisheria.
“Mahakama itafanya kazi yake na itatoa haki. Bunge halipo juu ya Katiba, Mahakama jukumu lake ni kutoa haki, Spika asidhani yeye yupo juu ya Katiba.”
Wiki iliyopita Spika Ndugai alilieleza Bunge kuwa wabunge waliosimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge (Mdee na Bulaya) hawatarudi bungeni kabla ya mwaka mmoja wa adhabu kuisha hata kama wataenda katika mamlaka zingine kudai haki.
There Goes my girl , see u shine errr day