Halima Mdee, Mbunge wa jimbo la kawe (Chadema) ameituhumu Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu nchini (HESLB) kwa kufanya ubaguzi wa elimu, anaandika Hellen Sisya
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari, mbunge huyo amesema kuwa miongoni mwa sifa za waombaji ambazo zimeainishwa na bodi hiyo ni za kibaguzi ikiwemo kigezo namba 10 ambacho kinawataka waombaji ambao wazazi wao ni viongozi wa umma au kisiasa ambao wanatajwa na sheria ya maadili ya viongozi wa umma kutokuomba mikopo.
Kwa mujibu wa mbunge huyo, hata madiwani ambao hawana mshahara nao pia wanatajwa na sheria hiyo, hivyo kuwakataza watoto wao kuomba mikopo ni kuleta ubaguzi katika elimu.
“Kwa watu wa kawaida wakisikia watu wanaojaza fomu za maadili, wanajua labda ni ngazi za ubunge na mawaziri. Lakini pia hata katika hizo ngazi za ubunge, ama mawaziri, ama mkurugenzi,unamnyimanye mtu haki yake ya kikatiba, ya mtoto wake kupewa fursa ya elimu sambamba na mikopo, kwa kudhani kwamba huyu mtu mwenye nafasi hiyo, basi ana uwezo wa kulipa. Unajuaje kama analipia watoto 10 au 20 kwa mwaka?” alihoji Mdee
Kwa mujibu wa mbunge huyo, serikali inatumia hoja nyepesi na ambazo hazina mashiko kuleta ubaguzi katika sekta ya elimu,jambo ambalo wao kama chama watalikemea.
Leave a comment