IMEELEZWA kuwa upungufu wa majengo ya kutolea tiba pamoja na vyumba vya kulaza wagonjwa katika hospitali ya wilaya ya Mbozi ni miongoni mwa mambo yanayochangia wagonjwa kulala wawili hadi watatu katika kitanda kimoja, anaandika Mwandishi Wetu.
Kauli hiyo ilitolewa na Mbunge wa viti maalum (CCM) Juliana Shonza katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa mpira wa miguu uliopo mjini Vywawa ambapo alimuomba Waziri Mkuu kuwasaidia ili waondokane na shida hiyo.
Alisema hospitali hiyo imekuwa ikihudumia wakazi wa wilaya zaidi ya 300 na wengine wanatoka nchi jirani ya Zambi hivyo inakabiliwa na changamoto nyingi kutokana na kupokea wagonjwa wengi kuliko uwezo wake.
Naye Mbunge jimbo la Vwawa, Japhet Hasunga kupitia mkutano huo alimuomba Waziri Mkuu kutoa idhini ya ujenzi wa hospitali ya mkoa kujengwa eneo la Ilembo kwa kuwa ofisi za mkoa zimeanza kujengwa eneo la Selewa na Mbozi ijengwe Manispaa.
Alisema wakati wa kutafuta eneo la kujengwa ofisi za mkoa kulileta malumbano makubwa ambapo kila upande ulivutana, lakini baada ya serikali kupitisha eneo hilo la Selewa sasa tumetulia na sasa ombi letu wana Vywawa ni hospitali ya Mkoa ijengwe Ilembo.
Akijibu maombi hayo Waziri Majaliwa, alisema tayari serikali imetenga fedha kwa ajili ya kujenga hospitali ya wilaya kwa wilaya zote ambayo hazina hospitali na kuwa tatizo la ukosefu wa vyumba vya kulaza wagonjwa litapatiwa ufumbuzi kwa kuwa tayari serikali imeleta fedha.
Leave a comment