MBUNGE wa upinzani katika jimbo la Kawe, jijini Dar es Salaam, Halima James Mdee, anashikiliwa na jeshi la polisi nchini. Anatuhumiwa kutoa kauli za kashfa dhidi ya Rais wa Jamhuri, Dk. John Pombe Magufuli. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum Dar es Salam, Lazaro Mambosasa, amethibitisha kukamatwa kwa mwanasiasa huyo.
Amesema, “Mdee anamshikilia kufuatia kauli yake aliyoitoa katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Kata ya Mikocheni, tarehe 21 Februari 2019.”
Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE, wakili wa Mdee, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (BAWACHA), Hekima Mwasipuanasema, mteja wake anashikiliwa na Polisi kwa madai ya kutoa kauli za uchochezi.
Anasema, “Mdee alipokea wito wa kutakiwa kufika kwenye ofisi ya mkuu wa upelelezi Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni (RCO). Alitekeleza agizo hili. Alifika kituoni hapo saa 3 asubuhi.”
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya Chadema, kauli ambayo Mdee anadaiwa kuitoa, ni ile inayokejeli ununuzi wa ndege.
Mdee anatuhumiwa kuwa alipokuwa kwenye mkutano wa hadhara katika Kata ya Mikocheni, tarehe 21 Februari 2019, alitoa kauli yenye lengo la kumgombanisha rais na wananchi.
Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE, Hekima amesema, “Mdee aliwasili polisi saa 3 asubuhi na baada ya mahojiano, polisi wakaamua kumnyimwa dhamana.”
Mwasipu amesema, madai yanayoelekezwa kwa Mdee ni kwamba alisema “mtu ananunua ndege badala ya vifaa vya zahanati, hii ni akili au matope.”
Leave a comment