MBUNGE wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (CCM), Jaku Hashim Ayoub amehoji sababu za mbwa kutumika kwa ukaguzi wa vyakula na watoto wadogo katika bandari ya Dar es Salaam kwenda Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Katika swali lake aliloliuliza leo Ijumaa tarehe 15 Mei, 2020 kwa wizara ya ujenzi, uchukuzi na mawasiliano na kujibiwa kwa njia ya mtandaoni na wizara hiyo, Ayoub amesema Serikali haina dini, lakini imekuwa ikiheshimu sana madhehebu ya dini.
“Namshukuru, Rais kwa hili; hivi karibuni katika bandari ya Dar es salaam wananchi waliokuwa wakisafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Zanzibar walikutana na kadhia kubwa sana ya mizigo, watoto wao na vyakula vya watoto kunuswa na mbwa,” amesema Ayoub na kuhoji;
(a) Je, ni sababu gani iliyosababisha mizigo, watoto wadogo na vyakula vyao kunuswa na mbwa;
(b) Je, Bandari ya Dar es Salaam haina X-Ray mashine na ulinzi wa kutosha;
(c) Je, ni lini tabia hiyo itakoma.
Akijibu swali hilo, waziri wa ujenzi, uchukuzi na mawasiliano amesema, zoezi la ukaguzi wa mizigo kwa kutumia mbwa wa kunusa linafanyika katika bandari ya Dar es Salaam katika maeneo mbalimbali ikiwemo eneo la huduma ya abiria.
Zoezi hili linafanyika sambamba na ukaguzi wa mashine X-ray baggage scanner na ukaguzi mwingine wa kawaida (physical inspection).
“Ukaguzi wa mizigo kwa kutumia mbwa wa kunusa hulenga kubaini nyara za serikali na madawa ya kulevya na hufanyika kwa mizigo ambayo haiwezi kukaguliwa katika midaki ya kukagua mizigo (X-Ray baggage scanner). Mizigo inayokaguliwa kwa mbwa haihusishi watu na vyakula, ambao hukaguliwa katika midaki,” amesema waziri
Amesemabandari ya Dar es Salaam inazo mashine za ukaguzi wa mizigo za X-Ray na pia ulinzi ni wa kutosha.
“Ukaguzi wa mizigo hususan mizigo ambayo haiwezi kukaguliwa katika midaki ya mizigo magetini yenye viashiria vya kuwa na nyara na madawa ya kulevya utaendelea kufanyika kwa lengo la kubaini, kuzuia na kudhibiti uhalifu bandarini,” amesema
Leave a comment