VIONGOZI waandamizi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) leo tarehe 14 Machi 2019 wamesomewa upya mashtaka yao kutokana na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kupangia hakimu mwengine katika kesi yao ya uchochezi. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Awali Kelvin Mhina, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo alisema kuwa, kesi hiyo itapangiwa hakimu wa kuendelea kuisikiliza baada ya kumaliza kusikiliza rufaa iliyotokana na kufutiwa dhamana kwa mshitakiwa namba moja, Freeman Mbowe na mshtakiwa namba tano Ester Matiko.
Rufaa hiyo ilifutwa tarehe 23 Novemba mwaka 2018 na Jaji Wilbard Mashauri akiwa Hakimu Mkazi kwenye mahakama hiyo.
Tarehe 7 Machi Jaji Sam Rumanyika alitoa hukumu ya kuwarejeshea dhamana zao Mbowe na Matiko ambapo katika hukumu hiyo aliamuru usikilizwaji wa haraka wa kesi ya msingi kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Katika kesi ya msingi yenye mashtaka 13 mbali na Mbowe Mwenyekiti wa Chadema –Taifa na Matiko, Mbunge wa Tarime mjini wengine ni Peter Msigwa Mbunge wa Iringa Mjini , Salum Mwalimu Naibu Katibu Mkuu Chadema Zanzibar.
Wengine ni pamoja na John Mnyika, Mbunge wa Kibamba; Vicent Mashinji, Katibu Mkuu Chadema-Taifa, Halima Mdee, Mbunge wa Kawe; John Heche, Mbunge wa Tarime vijijini na Ester Bulaya, Mbunge Bunda Mjini.
Leo Tarehe 14 Machi, 2019 Hakimu Mkazi Thomas Simba amepokea kesi hiyo na kueleza kuwa, kabla hajaendelea na usikilkizaji wa kesi hiyo ni vema watuhumiwa wakasomewa mashtaka ili asiruke hatua kwenye uendeshaji wa kesi hiyo.
“Hii kesi ilikuwa ikisikilizwa na hakimu ambaye kwa sasa hayupo kwenye nafasi hiyo ….hatua hiyo ya kisheria ni muhimu ikirukwa kesi ikiisha endapo itafika juu itarejeshwa chini kwa maneno machache,” amesema Hakimu Simba.
Upande wa Serikali uliongozwa na Wakili Mwandamizi Wankyo Simon huku upande wa utetzi ukiongozwa na wakili Profesa Abdallah Safari akisaidiwa na Mutabesya, John Mallya na Peter Kibatala.
Wankyo amesoma upya mashtaka yale yale kwa watuhumiwa wate tisa ambapo alipomaliza kusoma mashataka hayo aliiambia mahakama kuwa upande wao upo tayari kwa usikilizaji na kwamba italeta mashahidi wao makamani hapo.
Mashtaka yanayowakabili watuhumiwa hao ni pamoja na ambapo wakili Wankyo amesema kosa la kwanza limefanya na watuhumiwa wote tisa ambalo ni kula nyama ya kufanya mkusanyiko usio hahali, kufanya mkusanyiko ama maandamano yasiyo na uhalali Februari 16, 2018 katika barabara ya Mkwajuni kwa lengo la kuwaogopesha watu waliokuwepo eneo hilo.
Kosa la pili linalomkabili Mbowe ni kuwa, inadaiwa tarehe 16 Februari 2018 ni kuendelea kufanya mkusanyiko usio halali, shitaka ambapo linawakabili washtakiwa wote wakidaiwa kutenda kosa hilo Februari 16, 2018 katika Barabara ya Kawawa maeneo ya Kinondoni, Mkwajuni.
Viongozi hao kwa pamoja na watu wengine 12 ambao hawajafikishwa mahakamani wakiwa katika maandamano na mkusanyiko wa vurugu, waligoma kutii amri ya kusambaratika na kuvunja mkusanyiko huo uliosababisha kifo cha Akwilina Akwiline na majeraha kwa maofisa wa polisi.
Kosa lingine linalomkabili Mbowe ni uchochezi na kusababisha chuki katika jamii, ambapo inadaiwa alitenda Februari 16, 2018, akiwa Uwanja wa Buibui Kinondoni, Dar es Salaam akihutubia wakazi hao alitoa matamshi ambayo yangepelekea chuki katika jamii.
Mbowe anadaiwa kufanya kosa la uchochezi wa uasi, ambapo inadaiwa amelitenda Februari 16, 2018 katika viwanja vya Buibui, Kinondoni, Dar es Salaam alipotoa matamshi ambayo yangepandikiza chuki na dharau kwa wananchi wa Tanzania dhidi ya uongozi uliopo madarakani.
Kosa la saba linamkabili Mbowe ambalo ni ushawishi wa utendekaji wa kosa la jinai, ambalo amelitenda Februari 16, 2018 maeneo ya Buibui Kinondoni, Dar es Salaam, akiwa amejumuika na watu wengine aliwashawishi wakazi wa maeneo hayo na DSM kutenda kosa.
Wakili Wankyo amedai kosa la nane, linamkabili Msigwa ambalo ni kushawishi raia kutenda kosa la jinai, alilotenda Februari 16, 2018 katika viwanja vya Buibui Kinondoni, Dar es Salaam, ambapo aliwashawishi wakazi wa maeneo hayo na DSM kutembea mbele ya umma wakiwa na silaha.
Leave a comment