JAMES Mbatia, Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi amesema amekutana na Rais John Magufuli na kumuuliza, hatima ya Tanzania. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 3 Machi 2020, katika Makao Makuu ya chama hicho jijini Dar es Salaam, Mbatia amesema Rais Magufuli aliwawaita wapinzani ili kuzungumzia masuala ya mbalimbali ya kitaifa.
“Leo nimeitwa na rais, alikuwa anaongea na viongozi wa vyama mbalimbali vya siasa. Nikamuuliza, nchi hii tunaipaleka wapi?
“Akaniambia, anaendelea kusisitiza, uchaguzi wa mwaka huu utakuwa huru na haki, kama vyama vya siasa tukae chini tuzungumze tuweke kanuni sheria na utaratibu,” amesema.
Amesema, ametumia nafasi hiyo kumkumbusha rais kuhusu masuala ya maridhiano, masuala ya Watanzania na wadau wa siasa kukaa pamoja na kutosahau kwamba binadamu wote ni ndugu.
Hata hivyo, Mbatia ameeleza kusikitishwa na namna yeye na chama chake wanavyoporomoshewa matusi kutokana na itikadi ya chama hicho ya utu.
Mbatia amedai, watu wanaomtukana pamoja na chama hicho ni wale ambao wanapingana na fikra za NCCR-Mageuzi, na kuwa hawatojibu matusi hayo kwani chama hicho kina haki ya kuwa na fikra tofauti na wengine.
“Yameanza kutokea matusi ya yanayo dhalilisha sana, natukanwa sana lakini kama ni matusi hayanipi shida sana, leo tunatukanana na hakuna wakukemea matusi haya, tuna haki ya kuwa na fikra tofauti na wengine,” amesema na kuongeza:
“Wale ambao wanajaribu kwenda kinyume na msimamo wetu wa itikadi yetu ya utu, ni bahati mbaya sana na inasikitisha japo wanatutukana wao kwasababu ya itikadi yetu ya utu, sisi hatutawarudishia matusi. Tutazungumzia misingi endelevu ya kuliunganisha taifa letu.”
Leave a comment