WATU wawili, Judith Amoni Mwansansu (39) Mkazi wa Mwanjelwa na Aive Alex Swalo (17) Mkazi wa Mwanjelwa Mtaa wa Soko wanashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kosa la kumfanyia vitendo vya ukatili mtoto wa miaka sita. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 1 Agosti, 2018 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, SACP Ulrich Matei amesema tukio hilo lilifanyika jana majira ya saa tatu usiku ambapo jeshi la polisi lilipokea taarifa za tukio hilo kutoka kwa raia wema, ya kwamba mtoto huyo amejeruhiwa sehemu mbalimbali kwa moto.
“Inadaiwa kuwa siku hiyo ya tukio mhanga alikuwa ameenda kucheza na rafiki zake na aliporudi nyumbani majira ya jioni ndipo shangazi yake alimuadhibu kwa kumchapa na waya wa umeme sehemu mbalimbali za mwili wake na kumsababishia majeraha na maumivu makali mwilini,” amesema Kamanda Matei na kuongeza.
“ Inadaiwa kuwa tarehe 01.08.2018 majira ya asubuhi, watuhumiwa waliendelea kumfanyia vitendo vya ukatili mtoto huyo kwa kumuunguza kwa moto sehemu za miguuni na kwenye makalio.”
Kamanda Matei amesema Mhanga amelazwa katika Hospitali ya Rufaa Mbeya kwa matibabu zaidi ya kitabibu huku watuhumiwa wote wawili wamekamatwa kwa mahojiano zaidi kuhusiana na tukio hilo.
Leave a comment