WATU kadhaa wameuawa Kaskazini Mashariki mwa Nigeria baada ya wanamgambo wa Boko Haram kushambulia vijiji vya Wakristo na kuteketeza Kanisa wakati wa Mkesha wa Krismasi. inaripoti BBC…(endelea).
Vyanzo vya habari katika eneo hilo vinasema, karibu watu wa 11 wameuawa.
Wapiganaji waliingia Pemi katika Jimbo la Borno, kwa kutumia magari na piki piki na kuanza kufyatua risasi holela.
Pemi iko karibu na Chibok ambako wasichana 200 wa shule walitekwa mwaka 2014.
Boko Haram wamefanya mashambulio kadhaa Kaskazini mwa Nigeria ambako wanapigana kupindua serikali ili kubuni taifa la Kiislamu.
Wanavijiji walitorokea msituni na baadhi yao bado hawajulikani waliko.
“Magaidi waliwaua watu saba, kuchoma moto nyumba 10 na kuiba bidhaa za chakula ambazo zilikuwa zigawanyiwe wakaazi wakati wa sherehe ya Krismasi ,”kiongozi wa wanamgambo Abwaku Kabu alisema.
Wasambuliaji walichoma moto kanisa, kumteka mchungaji na kuiba bidhaa za matibabu katika hospitali moja kabla ya kuiteketeza moto.
Mzozo wa Boko Haram ambao umedumu kwa miongo kadhaa, umesababisha mauaji ya watu karibu 36,000 na wengine milioni mbili kufurushwa makwao, kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa.
Leave a comment