WIZARA ya Nchi Ofisi wa Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imeeleza, watumishi wa sekta ya ardhi waliokuwa chini ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI, wamehamishiwa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Na kwamba, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imeanzisha Ofisi za Ardhi katika mikoa yote 26 ya Tanzania Bara kutoka Kanda tisa zilizokuwepo ili kusogeza huduma za sekta karibu zaidi na wananchi.
Wizara hiyo imetoa maelezo hayo baada ya Ester Matiko, Tarime Mjini kutaka kujua, Je, ni lini serikali itapeleka wataalam wa kutosha katika Halmashauri ya Mji wa Tarime, ili kuweza kupima ardhi kwa kata zate sita zilizosalia ili wananchi hao waweze kunufaika na ardhi yao?
Amesema, ili ardhi iwe na thamani lazima ipimwe ili kupelekea wafanyabiashara na wakulima kupata mikopo katika taasisi za fedha na kujiingizia kipato.
Ndani ya jimbo la Tarime Mjini, kata mbili tu za Bomani na Sabasaba ndizo zimepimwa ardhi kwa asilimia 75 kati ya kata nane za Halmashauri ya Mji wa Tarime, na hii ni kutokana na upungufu mkubwa wa wataalam wa kupima ardhi.
Wizara imefafanua, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi imepanga watumishi wa kada zote katika ngazi za mikoa ambao watafanya kazi za kuidhinisha michoro ya upangaji miji, ramani za upimaji ardhi, uthamini, umilikishaji wa ardhi pamoja na usajili wa hati na nyaraka mbalimbali.
“Watumishi hawa wamesharipoti kwenye vituo vyao vya kazi. Hatua inayoendelea ni kuwapanga watumishi hao kwa kuzingatia uwiano kwa kada zote za maofisa ardhi wakiwemo maofisa mipangomiji, wapima ardhi, warasimu ramani, wathamini na maofisa ardhi,” imeeleza wizara hiyo.
Leave a comment