AFISA masoko wa Jiji la Dodoma, James Yuna amewaonya baadhi ya wafanyabiashara ambao wanafanya utapeli kwa wafanyabiashara wenzao kwa kitendo cha kuwauzia maeneo ndani ya masoko kinyume na utaratibu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Yuna alisema kuwa ni marufuku kwa mfanyabiashara yoyote au dalali kumuuzia mfanyabiashara eneo la biashara katika ndani ya soko katika masoko yote yaliyopo Jijini Dodoma kwa maelezo kwa kwa kufanya hivyo ni kuwatapeli wafanyabiashara wenzake.
Mbali na hilo alipiga marufuku kwa baadhi ya wafanyabiashara ambao wamekuwa na tabia ya kuchukua maeneo ya biashara na kuyapangiza kwa watu wengine jambo ambalo alisema kuwa kwa kufanya hivyo ni sawa na kuendelea kufanya utapeli na kuwaweka wafanyabiashara hao waliopanga kuwa katika wakati mgumu zaidi.
Yuna alitoa maelekezo hayo katika kwa wafanyabiashara wa Stendi Mpya iliyopo Kizota, Jijini Dodoma ikiwa ni sehemu ya utendaji wake wa kazi wa kutaka kuhakikisha wafanyabiashara katika masoko yote ya Jiji la Dodoma yanatumiwa kama yalivyokusudiwa.
Yuna alilazimika kutoa kauli hiyo kutokana na kuwepo kwa malalamiko kati ya wafanyabiashara na baadhi ya uongozi wa soko kwa maelezo kuwa wapo baadhi ya viongozi ndani ya masoko wamekuwa wakiwauzia maeneo wafanyabiashara.
Mbali na kuzuia baadhi ya viongozi wa soko kuwauzia maeneo wafanyabiashara, Yuna amepiga marufuku vitendo vya baadhi ya wafanyabiashara kuchukua vibanda vya biashara na kuvipangisha kwa mtu mwingine.
Yuna alisema kuwa ndani ya masoko kumekuwepo na baadhi ya watu ambao wanajigeuza kuwa mataperi na kufanya udalali wa kuuza maeneo ndani ya soko jambo ambalo siyo sahihi.
“Nataka niwaambie nyie wafanyabiashara msikubali kutapeliwa na baadhi ya watu ambao wanajiita viongozi wa soko kwa lengo la kuwapatia maeneo au kuwapangisha vibanda, ni lazima mkatambua kuwa mwenye uwezo wa kupangisha kibanda cha biashara ni halmashauri ya Jiji.
“Ni marufuku kwa mtu yeyote kumuuzia mfanyabiashara sehemu ya soko au mfanyabiashara kumpangisha mfanyabiashara mwenzake ndani ya soko kwani kwa kufanya hivyo ni sawa na kufanya utapeli.
“Jambo lingine ambalo wafanyabiashara mnatakiwa kulijua ni kwamba mnatakiwa kufanya shughuli zenu za biashara katika maeneo ambayo yamepangwa kisheria sisi hatutaki mfanye biashara katika mazingira ambayo hayaruhusiwi na iwapo utafanya biashara katika maeneo ambayo ni hatarishi kama vile kutimia miundombinu ya barabara, maji na sehemu nyingine ni lazima utambue kuwa utakuwa umekiuka taratibu na sheria za masoko,” alisema Yuna.
Naye Diwani wa Kata ya Kizoto Jijini, Dodoma Jamali Ngalya (CCM) amekiri kuwepo kwa baadhi ya wafanyabiashara ambao wanafanya baishara katika masoko bila kufuata utaratibu huku akimwomba afisa masoko wa Jiji kuwapa siku saba tu wafanyabiashara hao kuwa wameondoka.
Leave a comment