Wednesday , 24 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Mashirika ya kimataifa yawalaani Magufuli, Makonda
Habari za SiasaTangulizi

Mashirika ya kimataifa yawalaani Magufuli, Makonda

John Magufuli, Rais wa Tanzania (kulia) akiwa na Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam
Spread the love

WADAU wa habari, mashirika ya haki za binadamu na asasi za kiraia zinazojihusisha na utawala wa kidemokrasia katika nchi mbalimbali duniani, zimetoa kauli ya kulaani vitendo vya ukandamizaji wa uhuru wa habari vinavyoendelea nchini Tanzania, anaandika Mwandishi Wetu.

Tamko lao linakuja kufuatia kikao cha siku mbili kilichoketi juzi na jana mjini Kampala, Uganda ambapo pamoja na mambo mengine walijadili hali ya uhuru wa kujieleza na upatikanaji wa taarifa katika nchi mbalimbali.

Katika tamko lao lililosainiwa na jumla ya mashirika, taasisi na asasi za kiraia 33 wamesema.

“Tunalaani kwa nguvu zote uvamizi haramu uliofanywa na Mkuu wa Mkoa ili kulazimisha kurushwa kwa kipindi ambao ndiyo umesababisha Waziri wa Habari kufukuzwa baada ya kuingilia na kuunda tume ya uchunguzi dhidi ya suala hilo.”

Itakumbukwa kuwa tarehe 17 Machi, mwaka huu saa nne na dakika 40 usiku, Paul Makonda (Daudi Albert Bashite) aliongoza uvamizi katika kituo cha utangazaji cha Clouds Media akiwa na askari sita wenye silaha, kilazimisha kurushwa kwa video inayohusu mwanamke anayedaiwa kuzaa na Askofu Josephat Gwajima.

Nape Nnauye, waziri wa habari alilaani tukio hilo baada ya kukitembelea kituo hicho na kuunda tume ya uchunguzi iliyoongozwa na Dk. Hassan Abbasi, Msemaji Mkuu wa Serikali. Hata hivyo Nape alifukuzwa kazi siku moja baada ya tume hiyo kukabidhi kwake ripoti iliyomtia hatiani Makonda.

“Vitendo vya mkuu wa mkoa, na kufukuzwa kwa waziri aliyepinga uvamizi katika kituo cha Clouds Media ni kinyume na sheria na Katiba ya Tanzania.

Tunamtaka rais wa nchi hiyo kuzuia uvamizi dhidi ya vyombo vya habari na hata kuvamia mashirika ya watetezi wa haki za binadamu,” imesisitiza taarifa hiyo.

Tamko la asasi za kiraia na wadau wa habari mbalimbali pia limelaani vitisho vya Rais John Magufuli dhidi ya vyombo vya habari visivyoandika kulingana na matakwa ya serikali na kusema kauli za vitisho za kiongozi huyo hazikubaliki.

“Rais Magufuli ameyatisha magazeti na TV zisizoripoti habari za serikali kama serikali inavyotaka. Tangu kuingia kwa utawala mpya, Tanzania imeshuhudia kuminywa kwa uhuru wa kujieleza na kuhatarishwa kwa uhuru wa wanahabari.

“Zaidi ya matukio 40 ya ukamataji na unyanyasaji wa wanahabari yameripotiwa kufanywa na na wakuu wa wilaya kwa kipindi kisichozidi miaka miwili,” imesema taarifa hiyo.

Miongoni mwa mashirika yaliyotoa tamko hilo la pamoja ni Shirikisho la kimataifa la wanahabari la Ubelgiji, taasisi ya vyombo vya habari vya Ghana, Chama cha waandishi wa habari wa Rwanda, chama cha waandishi wa habari wa Cameroon na kituo cha mafunzo ya vyombo vya habari Liberia.

Mengine ni Chama cha wanahabari wa Guinea, chama cha taifa cha wanahabari wa Tunisia, taasisi ya maendeleo ya sekta binafsi na za umma ya Nigeria, Mtandao wa Taifa wa Taasisi za Haki za Binadamu Kenya, taasisi ya haki ya kujua (right to know) ya Afrika Kusini.

 

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za SiasaTangulizi

Biteko ataja vipaumbele 7 bajeti nishati 2024/25

Spread the love  NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mwekezaji amwaga bil. 39 kujenga viwanda 3 vya uchenjuaji

Spread the loveKampuni ya Mineral Access System Limited (MAST) inayoiwakilishwa kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

Mpwa wa Magufuli mbaroni kwa kusambaza picha za utupu

Spread the loveJESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limewakamata...

Habari za Siasa

Serikali kuanzisha mradi wa Gridi ya maji ya Taifa

Spread the loveWaziri wa Maji, Jumaa Aweso amesema katika mwaka wa fedha...

error: Content is protected !!