Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Masheikh, Maaskofu wataka haki uchaguzi mkuu 2020
Habari za SiasaTangulizi

Masheikh, Maaskofu wataka haki uchaguzi mkuu 2020

Spread the love

TAASISI za dini nchini Tanzania- Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) zimetaka haki itendeke kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika Jumatano tarahe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Wamesema, haki ndio msingi wa amani na kwamba Tume ya Uchaguzi Tanzania (NEC), itekeleze wajibu wake wa kusimamia haki pasi na kusikiliza sauti kutoka katika chama chochote.

Msimamo huo umefikiwa juzi Jumanne tarehe 11 Agosti 2020 baada ya kufanya kikao cha pamoja jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya kujadili amani na utulivu kuelekea uchaguzi mkuu.

Kwenye kikao hicho ambacho pia kilijadili haki, wajibu wa kijamii na ushiriki wa wanachi katika uchaguzi huo, Askofu Augustino Charles, Kiongozi wa Jimbo Katoliki Zanzibar amesema, amani inajengwa kwa haki.

“Naamini kwamba amani inajengwa kwa haki, kunapokuwa na haki ambayo ndio msingi, amani itakuwepo. Amani tunayozungumzia wakati huu wa uchaguzi ni kwamba kila chama kiwe na nafasi sawa na kingine,” alisema.

Askofu Fredrick Shoo

“Kila chama ambacho kinataka kusimama kugombea, kiwe na haki sawa na wote na vyombo vyetu vya kusajili na kusimamia uchaguzi, visiwe vinapata amri kutoka katika chama kimoja. Vipate amri kulingana na sheria zilizopo,” alisema

Alisema Zanzibar kuwa vyama vingi lakini vyama vyenye nguvu ni kama viwili au vitatu hivyo kuvitaka kuhakikisha vinatumia lugha nzuri pasina kubezana.

Askofu Charles alitumia fursa hiyo kuvitaka vyombo vya habari kutenda haki kwa wagombea wote “mwanahabari anapaswa kuwa sawa kwa wote, wenye nacho na wasionacho, kutoa fursa sawa. Kutoa haki sawa kwa wote.”

Sheikh Hamis Mataka, Msemaji wa Bakwata kwenye hadhara hiyo alisema, mkutano huo unaangazia haki na wajibu wa kijamii na ushiriki wa wananchi katika uchaguzi mkuu ujao.

Padri Charles Kitima

“Tunahitaji amani kabla ya uchaguzi na baada ya uchaguzi. Viongozi wa dini ni wadai wa uchaguzi, wanasiasa viongozi wa uchaguzi, Tume ya Uchaguzi wadau wa uchaguzi, wapiga kura wadau wa uchaguzi, kila mmoja anapaswa kutenda wajibu wake.”

“Amani ni tunda la haki, kila mmoja ahakikishe anatenda haki. Kwa hiyo, Tume ya Uchaguzi ya Taifa, wao kama mahakimu tunawatarajia watende kazi zao kwa haki, watende kazi zao kwa uadilifu,” alisema Sheikh Mataka.

Askofu Fredrick Shoo, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) alisema, amani na utulivu kuelekea uchaguzi mkuu ni jambo la muhimu.

“Ningeliomba kwamba Tume ya Taifa ya Uchaguzi ijue imepewa dhamana kubwa sana na Watanzania, na wao ndio wenye kusimamia kwa uhuru, haki na uwazi ili uweze kwenda kwa utulivu.

“Maana yake ni kuhakikisha kwamba haki za wagombea wote pasipo kuangalia chama zinalindwa, lakini pia haki za wapiga kura zinalindwa, na hapa tume ya uchaguzi ina kazi kubwa sana,” alisema Askofu Shoo.

Askofu Augustino Charles

Pia, alisema, vyombo vya usalama vitakavyosimamia uchaguzi huo kuhakikisha unakwenda salama, wanao wajibu wa kuhakikisha wapiga kura na wanaogombea wanalindwa.

Naye Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Charles Kitima alisema “sisi kama Watanzania, tumeamua kupata uongozi kwa njia ya uchaguzi na ni jukumu la wananchi kuweka viongozi wanaowataka ili kuwatumikia.”

“Usawa wa vyama, wingi wa vyama ni Watanzania waliamua kuwa na vyama vingi na wananchi wana fursa sawa ya kupata habari za viongozi wote ili wajue sifa zao na wawachague,” alisema Padri Kitima

Alisema tangu uchaguzi wa kwanza uliohusisha vyama vingi mwaka 1995, “mpaka sasa kuna vitu tumesahau na ndiyo maana viongozi wa dini wanasema kumbukeni mwaka 1995 tuliwahi kusema hivi.”

Viongozi hao walisema, viongozi wa dini, serikali na siasa wanaowajibu wa kuhakikisha amani inadumu katika jamii kwa kuwa inapotoweka, waathirika wakubwa ni wanawake, wagonjwa, watoto na wazee.

Walitaka ili kulinda amani katika uchaguzi, wagombea watakaoshindwa, lazima wakubali matokeo huku mamlaka husika zikisimamia haki na amani kwa wote.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

KimataifaTangulizi

Mkuu wa majeshi Kenya afariki, Ruto atangaza maombolezo

Spread the loveRais wa Kenya, William Ruto ametangaza maombezo ya siku tatu...

Habari za SiasaTangulizi

Tanzania, Uturuki zanuia kukuza biashara, uwekezaji

Spread the loveSERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha...

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

error: Content is protected !!